AMINA KASHEBA Na NASRA KITANA
KOCHA wa timu ya taifa ‘Taifa Stars’, Miguel Gamondi, amefurahia kiwango cha timu yake dhidi ya Nigeria na kusisitiza kwamba bado wana nafasi kubwa ya kutikisa katika mechi zijazo.
Taifa Stars ilionyesha kiwango hicho katika mchezo wa kwanza wa kundi C wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025 uliopigwa katika Uwanja wa Fez nchini Morocco.
Katika mtanange huo ambao Taifa Stars ilikubali kichapo cha mabao 2-1, ilionyesha kiwango bora hasa katika kuzuia makali ya Nigeria iliyoongozwa na straika Victor Osimhen.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Gamondi alisema kikosi chake kilionyesha kiwango kizuri dhidi ya Nigeria ambayo ina wachezaji bora.
Gamondi alisema licha mechi hiyo kuwa ngumu, makosa madogo madogo yaliyofanywa na timu yake ndiyo sababu ya kichapo.
Alisema atahakikisha anarekebisha mapungufu yaliyojitokeza katika mchezo huo ili kupata ushindi katika mchezo ujao dhidi ya Uganda.
“Tumepoteza mchezo dhidi ya Nigeria kwa sababu ya makosa madogo, lakini bado tuna nafasi ya kufanya vizuri katika mechi zinazofuata tukianza na Uganda, tunaimani tutapata ushindi,” alisema Gamondi.
Naye nyota wa timu hiyo, Simon Msuva alisema siyo matokeo mazuri kwa upande wao lakini watahakikisha wanapambana kupata ushindi katika mechi ijayo.
“Siyo matokeo mazuri kwetu lakini tutahakikisha tunapambana katika mechi zinazofuata ili kupata ushindi kwani ni mechi muhimu kwetu tusonge mbele,” alisema.
WADAU HAWA HAPA
Wadau wa soka nchini wamesifu ubora wa kikosi hicho katika mechi dhidi ya Nigeria huku wakisema wanaamini Stars ina nafasi ya kufanya vyema.
Kiungo mshambuliaji wa zamani wa Simba na Taifa Stars, Zamoyoni Mogella alisema Stars ilicheza katika kiwango kikubwa, wachezaji walijituma na kuonyesha nidhamu kubwa ambayo imewapa nguvu ya kupambana katika mechi ijayo.
Alisema kama watacheza hivyo katika michezo miwili ya makundi iliyobaki nafasi ya kutinga hatua ya mtoano itakuwa wazi.
” Stars walicheza katika kiwango kikubwa ambacho kila Mtanzania alishangaa, nina imani kama wataendelea kucheza hivyo matumaini ya kutinga mtoano yatakuwepo.
“Wachezaji walicheza kwa nidhamu kubwa na kujituma, mpira ulikuwa unachezwa vizuri na pasi zilionekana muhimu wanatakiwa kupunguza presha na kutumia vizuri nafasi ambazo wanazipata kwa lengo la kupata matokeo,” alisema Mogella.
Aliyekuwa kocha msaidizi wa Pamba Jiji, Salvatory Edward, alisema jambo la muhimu ambalo Stars wanapaswa kuliongeza ni umakini katika eneo la lango lao kwa sababu hapo ndipo kunakuwa na hatari ya kufungwa.
“Gamondi ameona makosa ya wachezaji nina imani ataenda kuyafanyia kazi mchezo ujao watafanya vizuri, kiujumla Stars wamecheza vizuri na kupeana pasi nzuri ambazo kila mtanzania matumaini yangu amefurahi kuona kiwango chao kizuri,” alisema.




