ABDUL DUNIA Na NASRA KITANA
WAKATI mechi za mzunguko wa kwanza Ligi Kuu Tanzania Bara, msimu huu, zikimalizika mwisho mwa wiki, Teknolojia ya Usaidizi wa Video (FVS), imeelezwa inaweza kuwa tiba ya makosa ya waamuzi na kuleta usawa kwa timu katika kuamua matukio uwanjani.
FVS ilianza kutumika katika mechi ya Ngao ya Jamii, iliyochezwa wiki iliyopita visiwani Zanzibar kati ya Simba na Yanga na kuendelea kuwepo katika mechi za ligi kuu Bara.
Teknolojia hiyo imeonekana kuwa na tija kutokana na kuondoa utata katika baadhi ya matukio ambayo iwapo yangetolewa uamuzi tofauti, yangeacha taswira isiyofaa katika michuano hiyo.
Katika mchezo wa Ngao ya Jamii, FVS ilimsaidia mwamuzi kutoka mkoani Manyara, Ahmed Arajiga, kutoa kadi ya njano kwa beki Ibrahim Hamad ‘Bacca’, baada ya kupiga mpira kwa mkono katika lango la Simba.
Pia, ilifuta malalamiko ya wachezaji wa Simba waliodai penalti kufuatia straika wa Yanga, Peter Shalulile, kuokoa mpira kwa mguu karibu na kichwa cha mchezaji wa Simba, Bakari Msimu ‘ndani ya eneo la 18’.
Katika Ligi Kuu Bara, FVS imewasaidia waamuzi kuamua kwa usahihi baadhi ya matukio yaliyosababisha hali ya sintofahamu.
Miongoni mwao ni penalti iliyozawadiwa timu ya Polisi Tanzania dhidi ya Azam FC dakika za mwisho, kuruhusu bao la Namungo dhidi ya Yanga japo awali ilionekana kama nyota wa Namungo, Hubert Lukindo, aliotea na kuhalalisha kadi nyekundu aliyooneshwa beki wa Simba, David Kameta ‘Duchu’.
Kutokana na teknolojia hiyo kutumika katika michezo ya Ligi Kuu Bara msimu huu, UHURU limezungumza na baadhi ya wadau wa soka, ambao wamesema wanaamini FVS itapunguza au kuondoa makosa kwa waamuzi msimu huu.
MWENYEKITI WA TPLB
Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara (TPLB), Nassor Idrissa ‘Father’, alisema uwepo wa FVS utasaidia timu kupunguza malalamiko na ana imani hata makosa ya ‘kibinadamu’ ya waamuzi yatapungua.
“Kiukweli wazo la kuleta FVS katika mechi zetu za hapa za ligi ni jambo zuri, malalamiko yalikuwa mengi lakini kwa hivi sasa nina imani yatapungua na tutakuwa na ligi bora zaidi,” alisema.
Father alisema kutumika teknolojia hiyo viwanjani, inatokana na ongezeko la ubora wa ligi ya Tanzania.
KAIMU KATIBU TFF
Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Oscar Mirambo, alisema mfumo huo utapunguza vilio dhidi ya waamuzi na kuongeza thamani ya ligi.
“Shirikisho limekuja na mfumo wa FVS kwa lengo la kutaka kupunguza malalamiko kutoka kwa klabu zetu, ambayo yangeweza kuharibu taswira ya ligi, tumeona katika Ngao ya Jamii na mechi za ligi mzunguko wa kwanza imetumika na hatukuona timu yoyote ikishusha lawama, nina imani tumefanikiwa kwa asilimia fulani japokuwa ligi ndiyo imeanza,” alisema Mirambo.
Alisema mfumo huo utaichochea TFF kuzidi kupambana kukamilisha mfumo wa kusaidia waamuzi kwa njia ya video (VAR).
MWENYEKITI WA FRAT
Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Waamuzi nchini (FRAT), Emmanuel Chaula, alisema mfumo wa FVS utawaepusha waamuzi kupewa lawama za mara kwa mara.
“Mfumo wa FVS utaendelea kuwalinda na kuwapa heshima waamuzi, ambao walikuwa wakilaumiwa na mashabiki au wachezaji,” aliongeza Chaula.



