Na Mwandishi Wetu, MWANZA
SERIKALI imesema imedhamiria kuendelea kuimarisha afua za ukimwi nchini kwa kuboresha mazingira ya utekelezaji wa shughuli hizo, huku ikihimiza ushirikiano na wadau katika kuendeleza mapambano dhidi ya virusi hivyo.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dk. Jim Yonazi, alipotembelea na kujionea utekelezaji wa shughuli zinazotekelezwa na vikundi vya watu wanaoishi na maambukuzi ukimwi katika Wilaya ya Nyamagana, mkoani Mwanza.
Dk. Yonazi amesema serikali imeendelea kuboresha mazingira na kutenga bajeti inayosaidia kuratibu na kutekeleza afua za ukimwi nchini, huku ikishirikiana na wadau kufanikisha shughuli hiyo.
“Ushirikiano ni muhimu sana kwani, tunaamini unaweza kutuvusha katika mapambano dhidi ya VVU, ambapo tumeendelea kuunganisha nguvu,” alisema Dk. Yonazi.
Alieleza Ofisi ya Waziri Mkuu, yenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za serikali, itaendelea kuhakikisha vifaa na huduma zinatolewa kwa wakati na ubora kwa watu waishio na virusi hivyo, huku kanuni na taratibu za afya zikizingatiwa.
Dk. Yonazi ametumia jukwaa hilo kuiasa jamii kuendelea kupima afya kujitambua na kuchukua hatua za mapema endapo mtu atabainika ana maambukizi ya VVU, aweze kuishi kwa tahadhari na kuwalinda wengine.
Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Balandya Elikana, amesema mkoa huo umechukua hatua madhubuti kuimarisha mapambano dhidi ya ukimwi kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya afya na kamati za utekelezaji wa mikakati ya kuzuia maambukizi, huku wakihimiza upatikanaji wa huduma bora na elimu kwa jamii.
“Jamii inaendelea kuhamasishwa kupima afya kwa hiari na matumizi sahihi ya njia za kujikinga na maambukizi ya virusi vya ukimwi na kuendelea kushirikiana kwa karibu na mashirika na wadau wa afya kuboresha huduma za kinga na tiba,” amesema Elikana.
Naye, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Kheri Kagya, akiwasilisha taarifa ya hali ya ukimwi, amesema mkoa wa Mwanza una kiwango cha maambukizi ya VVU cha asilimia 4.7, ikilinganishwa na kiwango cha kitaifa cha asilimia 4.4, kwa mujibu wa matokeo ya Utafiti wa Kitaifa wa THIS 2022/2023.
Alisema kwa mujibu wa taarifa ya DHIS2 ya mwaka 2025/2026, mkoa wa Mwanza unakadiriwa una watu wanaoishi na VVU 112,685.
“Mkoa, kwa kushirikiana na wadau, umeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya VVU kwa kuhamasisha matumizi sahihi ya kondomu.
Katika kipindi cha mwaka 2025/2026, mkoa huo umesambaza kondomu 2, 265, 772 katika jamii, hususani sehemu za kulala wageni, baa, kumbi za starehe na kwenye mikusanyiko,” amesema.



