Na NJUMAI NGOTA,
Magu
WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wananchi wilayani Magu, mkoani Mwanza, wamemdhihirishia Mgombea Mwenza wa Urais kupitia CCM, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, kwamba wameelewa vizuri ahadi za siku 100 zilitolewa na Mgombea Urais CCM Dk. Samia Suluhu Hassan, iwapo atapewa ridhaa kuunda serikali.
Hayo yamejidhihirisha baada ya mamia ya wananchi na wanaCCM kujitokeza kumlaki Dk. Nchimbi wilayani humo na kuelezea kwa ufasaha ahadi hizo zilizotolewa na Dk. Samia katika mkutano wa uzinduzi wa kampeni uliofanyika viwanja vya Tanganyika Packers, jijini Dar es Salaam.
Awali, Balozi Dk. Nchimbi aliwaomba wakazi hao waeleze walivyomsikiliza Mgombea Urais wa Chama, Dk. Samia kuhusu kazi atakazozifanya siku 100 za kwanza atakapopewa ridhaa ya kuiongoza nchi.
Alitaja miongoni mwa kazi atakazozifanya Rais Dk. Samia ni ajira mpya kwa walimu 7,000 wa masomo ya sayansi na hesabu, kupiga marufuku kizuizi cha maiti hospitalini kwa sababu ya gharama, kuboreshwa kwa huduma za afya, bima ya afya kwa wote hususan makundi maalumu na ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Mwanza-Isaka.
Mengine ni ujenzi wa madarasa na kuongeza shule za msingi miongoni mwa ahadi zinazogusa maisha yao.
Baada ya maelezo ya wananchi hao, Balozi Dk. Nchimbi aliwaambia wananchi hao ameridhishwa na namna walivyoelewa ahadi za Dk. Samia na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2025/2030.
Akizungumzia mafanikio yaliyopatikana kipindi cha uongozi wa Rais Dk. Samia, wilayani Magu, Dk. Nchimbi amesema Ilani imetekelezwa kwa mafanikio makubwa.
Ameyataja mafanikio hayo ni kuongeka kwa vituo vya afya kutoka vitano hadi saba, zahanati kutoka 34 hadi 43, huku vituo vya upasuaji magonjwa ya dharura vikiongezeka kutoka viwili hadi vitano.
Pia, shule za sekondari zimeongezeka kutoka 21 hadi 41 na madarasa kutoka 268 hadi 780, huduma ya maji imeongezeka kutoka asilimia 53 hadi asilimia 63, huku vijiji vinavyopata maji vikiongezeka kutoka 44 hadi 73.
Amesema upatikanaji wa umeme umeongezeka kutoka vitongoji 121 hadi 136, miradi ya umwagiliaji imefikia 12, majosho 19, mabwawa 145 na vizimba vya samaki kutoka 32 hadi 109.
Katika sekta ya miundombinu, barabara za lami zimeongezeka na kufikia kilometa 175 hali ambayo imefanya Magu kuwa mfano wa maendeleo vijijini na mijini.
Balozi Dk. Nchimbi alisema endapo yeye na Rais Dk. Samia watapewa ridhaa ya kuongoza kwa muhula wa pili, watahakikisha mafanikio yaliyopatikana kipindi cha miaka minne ya Rais Dk Samia yanaimarishwa na kuongezwa maradufu, hususan sekta za elimu, afya, miundombinu, maji na umeme vijijini.
Akiwa Kisesa, Balozi Dk. Nchimbi, alisema serikali imejenga kituo cha afya, kuongeza madarasa katika shule ya msingi, kujenga maabara na huduma ya maji kutoka asilimia 44 hadi asilimia 73.
ameongeza kuwa, wananchi 73 kati ya 100 wanapata majisafi na salama, huku shule za sekondari na msingi zikiboreshwa.
AZURU KABURI LA HAYATI NYERERE
Balozi Dk. Nchimbi amezuru kaburi la Hayati Mwalimu Julius Nyerere lililopo Butiama, mkoani Mara.
Dk. Nchimbi aliweka shada la maua katika kaburi hilo na kuwasha misumaa na kufanya ibada fupi na baadhi ya viongozi na wanafamilia wakiongozwa na mtoto wa Hayati Nyerere, Madaraka.




