Na MWANDISHI WETU
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Stephen Wasira, amesema wanachama walioongoza kura za maoni na kupewa dhamana ya kupeperusha bendera ya Chama katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, wana dhamana ya kuwaunganisha wana CCM na sio kuwafarakanisha.
Amesema CCM ni kama mtumbwi unaosafiriwa na wengine, hivyo, haitavumiliwa kuona watu wachache wanataka kuutoboa na kuzamisha watu wote.
Wasira, alieleza hayo, Kilombero mkoani Morogoro alipozungumza na Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM ya wilaya hiyo, akiwa katika ziara ya kutafuta kura za mgombea urais wa CCM, Dk. Samia Suluhu Hassan na wagombea ubunge na udiwani.
Alisema anatambua kuna msuguano, katika baadhi ya kata ambapo walioshindwa, wanasema hawajashindwa vizuri, hivyo kusababisha misuguano na walioshinda.
“Sisemi hapa mna matatizo makubwa, wala si kweli, yako majimbo yana matatizo, nimepitapita huko nimekutana na matatizo makubwa, kuna mahali imenibidi nifanye maamuzi magumu, hapa ninaambiwa matatizo hayo yapo ila yanaweza kumalizwa.
“Sasa ushauri wangu au niagize kwa wale walioshinda, ninyi mna dhamana zaidi ya kuleta umoja kuliko walioshindwa, kwa sababu ukishinda na wewe tena ukawa unatamba na watu wako nao wanawatambia wengine, unatufarakanisha,” alisema.
Alisema ushindi walioupata baadhi ya wana CCM kwa kuongoza kura za maoni, unatokana na mfumo uliojiwekea Chama kupata wagombea.
“Ule ushindi wa ndani ya Chama ni mfumo wa kupata mgombea, siyo mapambano ya kufanya wengine waonekane wanafaa na wengine hawafai, siyo kweli.
“Maana kuna mahali pengine hata aliyeongoza hatukumchukua tukamchukua wa pili, kuna mahali tukamchukua wa tatu,” alisema.
Aliwasihi waliopewa nafasi kuonesha njia katika kuleta umoja kwa walioshindwa kwa kuwa, wote ni wanachama wa CCM na uongozi ni zamu kwa zamu.
“Hivyo, kama ilikuwa zamu yenu kuongoza, basi ambao hawakuongoza na wao zamu yao itakuja.
“CCM sisi ni kama watu tunasafiria katika mtumbwi, usitoboe mtumbwi ambao tunasafiria wote, maana ukiutoboa, tunazama wote, kwa hiyo ukiongoza leo, utaongoza kwa miaka mitano, mtumbwi ule utakuwa bado upo kwa wengine nao kusafiria,” alisema.




