Na AMINA KASHEBA
UONGOZI wa Chama Cha Muziki wa Dansi Tanzania (CHAMUDATA), umewataka Watanzania kudumisha amani ya nchi kwani ndiyo nguzo muhimu ya kukuza siasa, uchumi na michezo.
Kauli hiyo, imetolewa jijini Dar es Salaam na Makamu Mwenyekiti wa CHAMUDATA, Angel Bushoke alipozungumza na UHURU kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuiunga mkono serikali.
“Unajua serikali yetu inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan inafanya mambo mengi makubwa, inapambana kwa nguvu zote kuhakikisha taifa linakuwa na amani, hivyo watanzania wanapaswa kuungana na kuwapuuza watu wenye kutaka vurugu,”alisema.
Angel alifafanua kuwa viongozi wa CHAMUDATA wana imani kubwa na i Tume Huru ya Uchunguzi ya Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu. uliofanyika Oktoba 29, mwaka jana.
Rais Dk. Samia aliunda tume hiyo, Novemba 18, mwaka jana kwa mujibu wa Sheria ya Tume za Uchunguzi ya mwaka 2023 (Sura ya 32) ambapo tume hiyo inaongozwa na Mwenyekiti, Jaji Mkuu Mstaafu, Mohamed Chande Othman.
“Tuseme kweli nchi ikiwa haina amani hakuna jambo litakalo fanyika, hivyo wananchi tunapaswa kushikamana na kama zipo changamoto zitatuliwe kwa hoja na si fujo.
“Wito wangu kwa Watanzania ni vyema tukaendelea kudumisha amani ya nchi yetu maana Tanzania tunasifika kuwa wakarimu ndiyo maana kuna baadhi ya watu wanatoka nchi zao na kuja hapa kwetu kuwekeza,” alisema.
Makamu Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa siku zilizopita zipo baadhi ya timu ziliomba kuja kucheza michezo yao hapa nchini kutokana na nchi zao kukosa amani.
“Hakuna jambo zuri kuona nchi yetu mwakani inakuwa moja ya nchi waandaji wa michuano ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika AFCON 2027, hii yote imetokana na kuwepo utulivu na amani,”alisema.




