Na MWANDISHI WETU,
Mwanza
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema shughuli za ufuatiliaji na tathmini ni nyenzo muhimu ya kuliwezesha Taifa kufanikisha na kufikia malengo mbalimbali ya kimaendeleo.
Amesema ni ukweli usiopingika, wadau wote na jamii kwa ujumla, wakiwa na uelewa wa pamoja kuhusu shughuli za ufuatiliaji na tathmini, matokeo ya haraka yatapatikana.
Majaliwa, alisema hayo katika Ukumbi wa Hotel ya Malaika Beach jijini Mwanza, alipomwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, katika ufunguzi wa kongamano la Nne la Kitaifa la Ufuatiliaji, Tathmini na Kujifunza.
Alisema serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali za kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji na tathmini, ikiwa ni utekelezaji wa vitendo, maono ya Rais Dk. Samia ya kuimarisha upimaji na utendaji wa Taasisi za Umma, uwajibikaji na kuongeza kasi na uwazi wa kutoa huduma na ustawi wa wananchi kwa ujumla.
“Shughuli za ufuatiliaji na tathmini, zinahusisha ukusanyaji, uchambuzi na upimaji wa taarifa kuhusu shughuli zilizopangwa, utekelezaji na matokeo yaliyopatikana.
“Serikali imekuwa na utaratibu wa kufanya shughuli hii katika vipindi mbalimbali,” alisema.
Katika hatua nyingine, Majaliwa alizitaka Idara zote zenye dhamana, zihakikishe zinakamilisha maandalizi ya Sera ya Taifa ya Ufuatiliaji na Tathmini kwa pande zote mbili za Serikali ili kuwezesha kutungwa kwa Sheria inayokwenda kuongoza Ufuatiliaji na Tathmini
Pia, aliziagiza Ofisi ya Waziri Mkuu na Mamlaka ya Serikali Mtandao, kukamilisha maandalizi ya Mfumo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini wa kielektroniki.
“Utakuwa mfumo mkuu wa mifumo yote ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji ndani ya serikali, lengo ni kuweza kuzifuatilia idara za serikali vizuri na utawezesha viongozi, watoa maamuzi na wananchi kupata taarifa na takwimu sahihi kwa muda.
“Watendaji wakuu wote tumieni taarifa zinazozalishwa kutokana na kazi za ufuatiliaji na tathmini ili mfanye maamuzi na kuweka mikakati imara ya kuhabarisha umma kuhusu matokeo ya utekelezaji wa kazi za Serikali kwa uhakika zaidi,”alisema.
Majaliwa alitoa rai kwa Chama cha Wataalamu wa Tathmini Afrika (AfrEA), kuendelea kuzilea TanEA (Tanzania) na ZaMEA (Zanzibar) kwa kuzipa uwezo zaidi wa kutekeleza majukumu yao ikiwemo kuwaongoza katika mabadiliko ya kiteknolojia ya utunzaji takwimu na ufuatiliaji.
“TanEA na ZaMEA, endeleeni kujiimarisha na kuongeza kasi ya kuwaunganisha wadau wote muhimu kwa lengo la kubadilishana mawazo na uzoefu au kujadili mbinu mpya na bora na zitakazowawezesha kuwafikisha kufanikiwa katika kufanya ufuatiliaji na tathmini wake,”alisema.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu, William Lukuvi, alisema katika jitihada za kuimarisha Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini nchini, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Mamlaka Mtandao – eGA imefanikiwa kuanza ujenzi wa mfumo wa Kitaifa wa Kielektroniki wa ufuatiliaji na tathmini ambao utapokea taarifa kutoka mifumo mingine na kuzichakata na kuwezesha maandalizi ya taarifa ya utendaji wa Serikali.
Naye, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Dk. Jim Yonaz, alisema serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu iliweka msingi imara wa kuimarisha shughuli za ufuatiliaji na tathmini kwa kuanzisha Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali.
Kwa Upande wake, Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, Suzan Ngongi, alisema uwazi na uwajibikaji umeiwezesha Tanzania kupiga hatua kubwa za kimaendeleo katika sekta za elimu, afya, miundombinu pamoja na mipango ya kupambana na umasikini.




