Na ATHNATH MKIRAMWENI
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amekemea tabia ya baadhi ya madereva wa magari ya serikali, kuvunja sheria za barabarani.
Ameagiza watakaokiuka, wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria.
Dk. Mwigulu, alisema sheria zilizowekwa kwa Watanzania, zisiwe na ubaguzi kati ya magari ya serikali na wananchi wa kawaida.
Kauli hiyo, aliitoa jijini Dar es Salaam, katika maadhimisho ya kwanza ya Wiki ya Usafiri Endelevu Ardhini yaliyobebwa na kaulimbiu; “Nishati Safi na Ubunifu katika Usafirishaji,” inayotoa mwongozo muhimu wa kuimarisha huduma za usafirishaji salama, bora na rafiki kwa mazingira.
Waziri Mkuu, alisema haikubaliki kuona sheria zinawakamata wananchi wa kawaida, lakini zikipuuzwa na baadhi ya viongozi au vyombo vya serikali.
“Baadhi ya watumiaji wa barabara, bado wanapuuza alama, hawawapi nafasi watembea kwa miguu na mara nyingine, huacha mawe katikati ya barabara baada ya matengenezo, hali inayoweza kusababisha ajali, tabia hizo ni kinyume cha uungwana na zinasababisha vifo visivyokuwa vya lazima,” alisema.
Alisema haikubaliki sheria zinawakamata wananchi wa kawaida, lakini zinapuuzwa na baadhi ya viongozi au vyombo vya serikali, kwa sababu sheria hizo, zimewekwa kwa Watanzania wote bila ubaguzi.
Alisema kuanzia sasa, hakutakuwa na mtu aliye juu ya sheria, hivyo wizara husika, Jeshi la Polisi na wadau wa sekta ya usafiri, wahakikishe sheria za usalama barabarani, zinatekelezwa bila upendeleo.
Dk. Mwigulu, alisema kama kuna kanuni au alama zilizopitwa na wakati, vyombo husika vya kutunga sheria, viangalie namna bora ya kuzibadilisha, zifuatwe na kila mtumiaji wa barabara.
Alisema miundombinu ya nchi siyo mali ya serikali au chama, ni mali ya wananchi kwa kuwa, imetengenezwa kwa fedha zao.
Dk. Mwigulu, aliwataka Watanzania kuitunza miundombinu hiyo kwa kuwa, ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa taifa, nchi jirani zinatumia bandari na barabara za Tanzania.
Aidha, alizitaka taasisi za serikali na sekta binafsi, kuongeza mafunzo kwa madereva, kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa vyombo vya usafiri, vikidhi viwango vya usalama.
Waziri Mkuu, alisema ukaguzi wa mara wa mara, utapunguza ajali na kulinda maisha ya abiria, mizigo na watumiaji wengine wa barabara.
Aidha, aliwapongeza wataalamu na watendaji wa sekta ya usafiri kwa kazi wanayoifanya, kuendeleza uchumi wa taifa.
Alisema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, anatambua mchango wa sekta ya uchukuzi kama damu inayoendesha mfumo wa mwili wa taifa.
Vilevile, alisema matumizi ya teknolojia mpya na nishati mbadala kama umeme, gesi na jua, yataboresha ufanisi na kupunguza gharama za usafiri.
WAZIRI MBARAWA
Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, alisema serikali inaendelea kusukuma mbele matumizi ya nishati safi katika miradi mikubwa ya uchukuzi.
“Reli ya Kisasa (SGR), inatumia umeme, mradi wa mabasi ya mwendokasi awamu ya pili, unaotumia gesi asilia na ongezeko la magari madogo ya teksi na pikipiki za magurudumu matatu yanayotumia gesi,” alisema.
Mbarawa, alisema mwelekeo huo ni rafiki kwa mazingira, hivyo aliwakaribisha wadau wa ndani na nje, kuungana na serikali kusukuma mbele matumizi ya teknolojia bunifu na nishati safi.
LATRA
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa wa Mamlaka ya Udhibiti, Usafiri Ardhini (LATRA), Habib Suluo, alisema sekta ya usafirishaji nchini, imepiga hatua kubwa kupitia uboreshaji unaoendelea chini ya Serikali ya Awamu ya Sita.
Suluo alisema Rais Dk. Samia, ameweka mazingira rafiki kwa wasafirishaji na kurejesha utulivu katika sekta hiyo, ikiwemo kuruhusu safari za saa 24 kwa mara ya kwanza baada ya zaidi ya miaka 20.
Alieleza mageuzi makubwa ya kidijitali yameongeza uwazi na usalama katika usafirishaji, kupitia LATRA App, abiria wanachagua basi, kufuatilia mwendokasi, vituo na ratiba za safari kwa kutumia simu zao.
Aliongeza polisi zaidi ya 60, wamekabidhiwa vifaa vya kufuatilia magari kwa muda halisi, hatua inayosaidia kudhibiti uvunjaji wa sheria na kupunguza ajali.
Alisema LATRA imeimarisha utambuzi na usajili wa madereva, wahudumu wa mabasi, kuongeza ubora wa huduma ambapo kila mhudumu, hutambuliwa kupitia mfumo wa mamlaka na madereva wakifuatiliwa kwa njia ya kidijitali.
Siku ya Usafiri Endelevu Duniani imeazimishwa nchini kwa mara ya kwanza mwaka huu, kufuatia Azimio Namba 77/286 la Umoja wa Mataifa.
Katika wiki ya maadhimisho, mijadala na maonesho, yanafanyika yakihusisha wadau wa usafiri wa barabara, majini, anga na Zanzibar, msukumo upo katika utunzaji mazingira, nishati safi na ubunifu wa sekta ya uchukuzi.




