>> Dk. Nchemba, Nape, Aweso, Jafo wamzungumzia
Na WAANDISHI WETU
MAKAMU wa Rais, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, anatarajiwa kuwaongoza waombolezaji katika misa ya kumuaga aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho (CCM), marehemu Jenista Mhagama.
Misa hiyo, inayofanyika leo katika Kanisa Katoliki, Parokia ya Kiwanja cha Ndege, jijini Dodoma.
Baada ya misa, waombolezaji watatoa heshima za mwisho, kisha mwili wa marehemu, utasafirishwa kupelekwa nyumbani kwake, Makambi wilayani Songea Mjini, Mkoa wa Ruvuma.
Maziko ya waziri huyo wa zamani, yanatafanyika Desemba 16 mwaka huu, Kijiji cha Ruanda, wilayani Mbinga,
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa juzi usiku na Ofisi ya Habari na Mawasiliano ya Bunge, ilieleza kuwa, Desemba 14 mwaka huu, mwili wa Jenista, utawasili mkoani Ruvuma.
Pia, itafanyika misa ya kumwombea katika Kanisa Katoliki, Matogoro, wilayani Songea.
Taarifa hiyo ilieleza zaidi kuwa, siku itakayofuata, mwili wa Jenista ambaye alihudumu kama waziri katika wizara mbalimbali, utasafirishwa kwenda Peramiho, Wilaya ya Songea Vijijini.
Desemba 16 mwaka huu, mwili wa marehemu utapelekwa Kijiji cha Ruanda, wilayani Mbinga ambako yatafanyika maziko.
SALAMU ZA DK. NCHIMBI
Akizungumza alipowasili nyumbani kwa marehemu, Itega jijini Dodoma, Makamu wa Rais Dk. Nchimbi, alisema taifa limepata pengo, kwani Jenista alikuwa kiongozi aliyeheshimika na kuitumikia nchi katika majukumu mbalimbali.
Alisema Jenista, licha ya kuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, alitoa mchango wake Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kusimamia maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma.
Makamu wa Rais, alitoa pole kwa familia na waombolezaji, huku akiwaomba watoto wa marehemu, ndugu, jamaa na waombolezaji, kuendelea na moyo wa ujasiri katika kipindi cha majonzi wanachopitia.
WAZIRI MKUU
Kwa upande wake, Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, alitoa salamu za pole kwa familia ya marehemu Jenista baada ya kufika kuhani msiba huo.
Alisema taifa limeshtushwa na kifo cha ghafla cha kiongozi huyo, akieleza kwamba, walikuwa pamoja bungeni siku chache zilizopita na kuonesha dalili zozote za matatizo ya kiafya.
“Tumeshtushwa sana na tukio hili la msiba, kwa sababu majuzi tu tulikuwa wote Bungeni, hakuwa akilalamika kuhusu masuala ya kiafya. Kwa hiyo tunamwachia Mungu,” alisema.
Dk. Mwigulu, alimwelezea marehemu Jenista kama kiongozi aliyekuwa na bidii, uwezo na uadilifu wa kutekeleza majukumu yake.
“Mheshimiwa Jenista tumefanya naye kazi kama mbunge na waziri. Ni mtu aliyekuwa na jitihada kubwa kuhakikisha kazi ambayo amepewa, inakuwa yenye matokeo. Alikuwa anataka mara zote kuona anatimiza wajibu kikamilifu,” alisema.
NAPE ASIMULIA KISA CHAKE NA JENISTA
Mbunge wa Jimbo la Mtama (CCM), Nape Nnauye, alielezea kumbukumbu alizonazo kumhusu Jenista.
Alisema urafiki wao ulianza kwa kugombana, tena ugomvi mkubwa, yeye akiwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Taifa huku Jenista wakati huo ni katibu wa wabunge wa CCM.
“Hakupenda msimamo wangu mkali dhidi ya serikali, mimi sikupenda msimamo wake wa wastani dhidi ya serikali.
“Hii ilipelekea tusielewane kabisa kwa muda kadhaa. Leo nimekumbuka kaseti ya nyimbo za kizalendo niliyoachiwa na Baba Marehemu Mzee Moses Nnauye, akamsalimie akimwona.
“Mwambie tungo ya nyimbo zake za kizalendo, hazijapata mshindani,” alisimulia mbunge huyo.
Aliongeza kuwa: “Nakumbuka nilipokuja Bungeni mwaka 2015, aliniuliza “Nape sasa unaelewa kwanini nilikuwa nachukia msimamo ule uliotugombanisha?.
Nikajibu: “Mama nakuelewa sana sasa.” Hapa na pale, nilipokuwa napandisha kidogo msimamo, alinirudisha kwa upendo ambao sitasahau malezi yake. Aaaah….nakumbuka ulipotufungia ofisini mimi na Bashe..!! Uliipenda kazi yako!!
“Kama binadamu, unaweza kuwa ulikuwa na mapungufu yako kama ilivyo kwa binadamu yeyote aliyezaliwa na mwanamke, lakini umetimiza wajibu wako kwa nchi yako,” alihitimisha.
ANNE KILANGO
Mbunge wa Same Mashariki (CCM), Anne Kilango Malecela, alisema kifo cha Jenista ni pigo kubwa kwao, akimtaja marehemu kama mbunge mchapakazi, ambaye alielewa vyema wajibu wa kazi, aliyetengeneza mazingira mazuri ya maelewano ndani ya Bunge.
Alisema hakuwahi kupata taarifa za ugonjwa wa Jenista na kwamba, habari za kifo zilimfikia moja kwa moja.
“Nilipopata taarifa, nililazimika kumpigia Spika wa Bunge, Mussa Azzan Zungu, ambaye alithibitisha taarifa hizo. “Niliumia sana kwa sababu, mimi na marehemu ni marafiki wa muda mrefu, tulioungana rasmi Bungeni mwaka 2000 kupitia CCM.
MBUNGE JAFO
Mbunge wa Jimbo la Kisarawe (CCM), Selemani Jafo, alisema Jenista alikuwa kiongozi mchapakazi mwenye kujitoa kwa taifa wakati wote wa utumishi wake.
Alibainisha kuwa, mchango mkubwa wa kiongozi huyo katika kusimamia na kuratibu majanga mbalimbali yaliyowahi kutokea nchini.
Alisema kuwa, alifanya kazi kwa ukaribu na Jenista katika matukio kadhaa makubwa yaliyotikisa nchi, ikiwemo ajali ya kuzama kwa kivuko cha Ukerewe, ajali ya mlipuko wa lori la mafuta mkoani Morogoro na tukio la maporomoko ya udongo Hanang mkoani Manyara.
Kwa mujibu wa Jafo, Jenista alikuwa shupavu, makini, mwenye moyo wa kuongoza kwa vitendo, hususan katika nyakati za majanga.
Katika salamu zake, Jafo alitoa rai kwa Watanzania, kuendeleza utamaduni wa kuwasifia na kuwapa heshima viongozi na watu muhimu wakiwa bado hai, akitoa mfano namna ambavyo aliwahi kumshukuru Jenista katika moja ya hotuba zake bungeni kwa mchango wake wa kulitumikia taifa.
KAULI YA DC SONGEA
Mkuu wa Wilaya ya Songea, Wilman Ndile, aliweka wazi mazungumzo yake ya mwisho na Jenista aliyofanya siku moja kabla ya kifo chake.
Alisema kabla ya kifo chake, marehemu Jenista alimtafuta kwa njia ya simu kumuuliza hali ya upatikanaji maji katika Kijiji cha Nakawale, Kitongoji cha Mkenda, kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.
Kwa mujibu wa Ndile, wananchi wa eneo hilo, wamekuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa ya upatikanaji maji safi kwa muda mrefu, ambapo baada ya kumweleza taarifa hiyo, mbunge huyo, aliahidi kurejea baada ya sikukuu ya Krismasi.
ANGELINA MABULA
Akizungumza na gazeti hili, aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula, alisema Jenista, alikuwa kiongozi mchapakazi, mwenye umakini katika utendaji na daraja la kuunganisha makundi mbalimbali.
Angelina, alisema Jenista alikuwa kiongozi mfuatiliaji wa mambo, asiyetaka jambo liharibike katika utumishi wake wote.
“Tumepoteza mtu mahiri, anayejituma, makini katika utendaji, alikuwa hataki mambo yaharibike, alikuwa kiongozi ambaye ana uwezo, wa kuwa daraja wa makundi mbalimbali.
MULAMULA
Naye aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberatha Mulamula, alisema Marehemu Jenista alilitumikia Taifa kwa nguvu kubwa na kuacha alama katika Wizara mbalimbali.
Alisema alipokea taarifa ya kifo cha Marehemu Jenista kwa mshtuko mkubwa, huku akiwaomba Watanzania kuendelea kumuombea.
AWESO
Naye Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, alisema Jenista, alikuwa kiongozi jasiri, shupavu na mhamasishaji mkubwa wa maendeleo ya Taifa.
Aweso, aliandika hayo jana kupitia mtandao wake wa kijamii wa Instagram, huku akiongeza kuwa, Jenista alikuwa kiungo muhimu kwa wabunge wengine, mzoefu na mzalendo.
“Nimepokea taarifa ya kifo cha Mbunge wa Peramiho Jenista Mhagama kwa mshtuko, masikitiko na huzuni kubwa sana.
“Tumeondokewa na kiongozi bora, katika nchi yetu na jamii yake wana Peramiho, kwani Mheshimiwa Mhagama alikuwa kiungo muhimu sana kwetu wabunge, kiongozi jasiri na shupavu, mzoefu, mzalendo kwa taifa lake na mhamasishaji mkubwa,”aliandika
MBUNGE SHIGONGO
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, Erick Shigongo akizungumza na gazeti hili jana, alisema Jenista alikuwa kiongozi muungwana, mkarimu na mwalimu wa wabunge wengi Bungeni.
Pia, alisema Jenista atakumbukwa kwa unyenyekevu, mshauri kwa wabunge wengi vijana.
Kwa mujibu wa Shigongo, Jenista alikuwa na mchango mkubwa sana kwake katika safari yake ya kurudi tena Bungeni kipindi cha pili, alikuwa mshauri wake wa nini afanye awe kiongozi bora na awemo katika mioyo ya wananchi wake.




