Na ATHNATH MKIRAMWENI
WAZIRI wa Maji, Juma Aweso, ameitaka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA), kugawa maji kwa usawa, uwazi na kutoa ratiba ya eneo husika, wananchi wapate muda wa kujiandaa.
Aweso, alisema hayo katika mkutano kati ya DAWASA na Wahariri wa Vyombo vya habari, kuzungumzia hali ya upatikanaji maji Jijini Dar es Salaam.
“Ni wazi kuna vitu vingine viko nje ya uwezo wetu ikiwemo kuchelewa kunyesha mvua ya vuli, lakini niwaombe wananchi tuendelee kuwa na mshikamano katika kipindi hiki cha mpito.
“Nasisitiza DAWASA, hiki kilichopo au tunachozalisha, gaweni maji hayo kwa usawa na uwazi kwa kueleza ratiba zenu ni saa ngapi, maji yatatoka katika eneo linalokusudiwa huduma hiyo, wananchi wajiandae kupokea hayo maji, kwa kufanya hivyo, itapunguza malalamiko kutoka kwa wananchi,” alisema.
Pia, alisema jambo hilo liwe shirikishi kwa watu wote, wakiwemo wadau wa sekta binafsi, watengeneze namna nzuri ya kugawa maji kwa kushirikiana na DAWASA katika visima vilivyochimbwa.
Pia, kutoa elimu kwa jamii juu ya namna ya kutunza vyanzo vya maji na kuepuka uharibifu wa mazingira.
MTENDAJI MKUU DAWASA
Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama Bwire, alisema upatikanaji maji katika Jiji la Dar es Salaam na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Pwani, umeendelea kukumbwa na changamoto kubwa kutokana na ongezeko la mahitaji.
“Takwimu za sensa ya mwaka 2022, zinaonesha eneo hili lina watu takribani milioni saba, huku idadi hiyo ikitarajiwa kufikia karibu milioni 17 ifikapo mwaka 2050 katika kipindi cha mwaka 2023–2026.
“Ongezeko hili limeongeza shinikizo kwa mifumo ya usambazaji maji iliyopo, ambayo tayari ilikuwa na upungufu hata kabla ya changamoto za msimu wa sasa,” alisema.
Alisema mahitaji ya maji, yamezidi kuongezeka siyo kwa sababu ya idadi ya watu pekee, bali kutokana na ongezeko la shughuli za kiuchumi na kubadilika kwa matumizi ya maji kwa kaya.
Akitolea mfano, alisema mtu aliyekuwa akitumia lita 40 kwa siku, sasa anatumia lita 60, hivyo kuongeza mzigo kwa mifumo ya uzalishaji.
Mtendaji huyo, alisema hadi sasa, uwezo wa uzalishaji upo katika lita milioni 534 kwa siku, asilimia 93 hutegemea vyanzo vya juu ya ardhi na asilimia saba, hutokana na visima.
Alisema kipindi hiki cha kiangazi, chanzo kikubwa cha maji hususan Mto Ruvu Chini, kimeathirika zaidi kutokana na upungufu wa mvua misimu ya vuli na masika.
Alieleza hali hiyo, imeshusha uzalishaji kutoka zaidi ya lita milioni 270 kwa siku, hadi takribani lita milioni 50 kwa sasa na kuathiri maeneo mengi ya utoaji huduma, yakiwemo ya Tegeta, Kawe, Mbezi, Kinondoni, Tabata, Kinyerezi na maeneo ya katikati ya jiji.
Alitaja sababu nyingine zinazochangia upungufu ni shughuli za kibinadamu ndani ya bonde la mto, ambazo zimebadilisha mikondo ya maji na kupunguza kiasi kinachofika katika mitambo ya uzalishaji.
Pia, kupanda kwa joto, kumesababisha uvukizaji mkubwa katika vyanzo vya juu ya ardhi, hali iliyosababisha kupungua kwa kiwango cha maji yaliyokuwepo.
Katika baadhi ya maeneo, mito midogo imetoka katika mkondo wake wa asili, hivyo kupunguza maji yanayoelekea katika chanzo kikuu.
Katika hatua za muda mfupi, DAWASA imeimarisha uchimbaji na ufufuaji visima katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo yake ya pembezoni.
Visima ambavyo awali vilikuwa vikizalisha lita milioni 17 hadi 20 kwa siku, sasa vinaboreshwa kufikia lita milioni 35 hadi 40.
Pia, maji kutoka visima hivyo, yanatumika kuimarisha huduma katika maeneo katikati ya jiji kama Kariakoo ili kupunguza utegemezi kutoka vyanzo vya juu ya ardhi.
“Kampeni za elimu kuhusu uhifadhi wa maji zinaendelea kutolewa kwa wananchi, wakihimizwa kuhifadhi maji kwa matumizi ya siku kadhaa kutokana na hali isiyotabirika ya upatikanaji wa maji.
“Hatua hizi, zimeanza kusaidia kupunguza ukubwa wa tatizo kwa kiwango fulani,” alisema.
Vilevile mtendaji, huyo alitaja hatua za muda mrefu ikiwepo serikali kuendelea kutekeleza ujenzi wa Bwawa la Kidunda, ambalo limefikia zaidi ya asilimia 35 ya kazi.
“Bwawa hilo, linatarajiwa kusaidia kudhibiti mtiririko wa Mto Ruvu, kuhakikisha upatikanaji wa maji katika vipindi vyote vya mwaka na kuzalisha megawati 20 za umeme.
“Miundombinu ya msingi ya kusafirishia maji tayari, imeanza kukamilika, hatua itakayowezesha mradi kuingia katika awamu ya kasi ya juu ya ujenzi,” alisema.
“Hatua ya kimkakati zaidi ni kuanzishwa kwa Mradi wa Maji wa Gridi ya Taifa, utakaotumia maji kutoka Mto Rufiji kuongeza uzalishaji wa zaidi ya lita bilioni 1.5 kwa siku ifikapo mwaka 2050.
Alisema mradi huo, utasaidia kuunganisha vyanzo vikubwa vya maji na kupunguza utegemezi wa chanzo kimoja na kuendelea kuchimba visima vipya katika maeneo ya pembezoni mwa jiji, kuimarisha upatikanaji wa maji.




