NA MWANDISHI MAALUM
TANZANIA imepongezwa kwa hatua kubwa ilizochukua katika kuzuia na kupambana na rushwa, hususan katika kuimarisha mifumo ya uzuiaji rushwa na utekelezaji wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa dhidi ya Rushwa (UNCAC).
Pongezi hizo zimetolewa jijini Doha, Qatar, wakati Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Crispin Chalamila, akiwasilisha taarifa ya Tanzania kuhusu utekelezaji wa Mkataba huo katika Mkutano Mkuu wa 11 wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa dhidi ya Rushwa.
Chalamila, ambaye anaongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo unaofanyika kuanzia tarehe 15 hadi 19 Desemba, 2025, alisema rushwa bado ni changamoto kubwa kwa mataifa mengi duniani kwa kudhoofisha utawala bora, kukwamisha ukuaji wa uchumi, kuongeza umaskini, kukiuka haki za binadamu na kudhoofisha taasisi za umma.
Ameeleza kuwa Tanzania imefanikiwa kuimarisha mifumo ya kuzuia rushwa kupitia utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa Kuzuia na Kupambana na Rushwa na Mpango wa Utekelezaji (NACSAP IV), pamoja na kuboresha mifumo ya manunuzi ya umma kupitia Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2023.
Aidha, nchi imeimarisha taratibu za urejeshaji wa mali zilizopatikana kwa njia za uhalifu ikiwemo rushwa, kupitia Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, sambamba na kuziimarisha taasisi simamizi zikiwemo TAKUKURU, Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Chalamila ameongeza kuwa, baada ya kukamilika kwa Mzunguko wa Kwanza wa Mapitio ya utekelezaji wa UNCAC uliofanywa na nchi za Austria na Msumbiji, Tanzania ilibainika kufanya mageuzi makubwa katika kuimarisha mfumo wa kitaifa wa kudhibiti uhalifu, utekelezaji wa sheria na ushirikiano wa kimataifa.
Mkutano Mkuu wa 11 wa Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa dhidi ya Rushwa hufanyika kila baada ya miaka miwili, ukiwakutanisha wakuu wa taasisi za kupambana na rushwa, watunga sera, viongozi wa kisiasa, asasi za kiraia, mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau wa maendeleo kutoka mataifa mbalimbali duniani.




