Na LATIFA GANZEL, Morogoro
JESHI la Polisi Mkoa wa Morogoro linamshikilia Rashid Paulo (35), mkulima na mkazi wa Msowelo kwa tuhuma za mauaji ya Steven Mayungu (26), mkulima na mkazi wa Mayungu.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Alex Mkama, alisema tukio hilo lilitokea, saa tano usiku katika Kitongoji cha Shuleni, Kata ya Lumuma, wilayani Kilosa.
Alisema uchunguzi wa awali umebaini mtuhumiwa alimchoma Mayungu na kitu chenye ncha kali eneo la kifuani, baada ya kutokea ugomvi kati yao unaodaiwa kusababishwa na wivu wa kimapenzi.
“Mtuhumiwa alimtuhumu Mayungu (marehemu) kuwa na mahusiano ya kimapenzi na mke wake,” alisema.
Alisema mtuhumiwa anashikiliwa na jeshi hilo kwa mahojiano zaidi huku utaratibu wa kisheria ukiendelea kufanyika.
Kamanda Mkama alitoa wito kwa wananchi kuepuka kujichukulia sheria mkononi, badala yake watumie vyombo husika kutatua migogoro au matatizo ya kifamilia kwa njia ya amani na kufuata sheria.
Wakati huo huo, dereva Uwimpue Bonheur (33), raia wa Rwanda, mkazi wa Kigali alikamatwa akiwa anaendesha gari la mizigo lenye namba za usajili RAI 878 G aina ya HOWO akiwa katika hali ya ulevi kipimo 171.7mg/100ml akitokea Kigali kwenda Dar es Salaam.
Kamanda huyo alisema tukio hilo lilitokea jana asubuhi katika eneo la Kwachambo, Manispaa ya Morogoro barabara kuu ya Morogoro- Dodoma.
Alisema mtuhumiwa alizuiliwa kuendesha chombo hicho kwa usalama wake na wadau wengine wa barabara wakati hatua zingine za kisheria zikiendelea.
Mkama aliwataka madereva kutotumia ulevi wakiwa wanaendesha magari kuepusha matukio ya ajali zinazogharimu maisha ya watu, uharibifu wa miundombinu na mali.




