NA MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, ametoa wito kwa viongozi wa dini kuendelea kushirikiana na serikali katika kutoa elimu ya umoja, amani, kupinga chuki, migawanyiko na vitendo vyovyote vinavyoweza kuvuruga mshikamano wa Taifa.
Amesema vita yoyote inayohusisha wenyewe kwa wenyewe huwa haina mshindi bali inawapoteza wote, huku akisisitiza mgawanyiko ndani ya taifa hauna mshindi bali una matokeo ya kushindwa wote kama Taifa.
Dk. Mwigulu alitoa wito huo aliposhiriki ibada ya Sikukuu ya Krismasi iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Kiinjili la Kilutheri la Azani Front jijini Dar es Salaam,
“Manufaa ya amani ni makubwa. Huleta maendeleo ya kiuchumi, huimarisha ustawi wa jamii na huwezesha kila Mtanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga Taifa,” alisema.
Alisema serikali inaendelea kutekeleza wajibu wake kulinda amani na usalama wa nchi, kuwajenga Watanzania na hususan vijana kuthamini dhana ya uzalendo kwa nchi.
“Tanzania imeendelea kuwa kielelezo cha umoja, amani, mshikamano na utulivu katika ukanda wetu na barani Afrika. Amani hii imejengwa juu ya misingi imara ya maadili, haki, kuheshimiana, uvumilivu na uzalendo,” alisisitiza.
Dk. Mwigulu alitoa wito kwa wazazi na walezi kuendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za elimu na dini katika kuimarisha malezi ya watoto na vijana kwa kuwajengea misingi imara ya maadili.
Katika Ibada hiyo, Dk. Mwigulu aliungana na Rais Dk. Samia, kuwatakia Wakristo na Watanzania wote heri ya Sikukuu ya Krismasi, huku akiwasishi kusherehekea kwa amani, upendo, utulivu, kudumisha mshikamano wa kitaifa kwa maslahi ya Taifa.
ASKOFU MALASUSA AKEMEA
Kwa upande wake, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili na Kilutheri Tanzania (KKKT) na Mkuu wa Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Askofu Dk. Alex Malasusa alikemea tabia za baadhi ya watu kuchafua taswira za watu wengine na kuichonganisha jamii.
“Kuna watu wakiona jamii imekaa pamoja kwa amani wao inawakosesha raha,”alieleza Askofu Malasusa.




