Na AMINA KASHEBA
BAADA ya kutopata matokeo mazuri katika mechi mbili za kwanza za kundi C Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2025, timu ya taifa ‘Taifa Stars’, imewekeza nguvu zake katika mchezo ujao dhidi ya Tunisia.
Taifa Stars itachuana na Tunisia kesho saa 1:00 usiku katika mtanange wa ‘kufa au kupona’ utakaopigwa katika Uwanja wa Prince Moulay Abdellah, Rabat nchini Morocco.
Katika mtanange huo, Tanzania inapaswa kupata ushindi wa aina yoyote kutinga hatua ya mtoano ya michuano hiyo mikubwa zaidi Afrika.
Hivi sasa, Tanzania ipo nafasi ya tatu katika kundi hilo ikiwa na alama moja sawa na Uganda inayoburuta mkia, kinra Nigeria yenye alama sita tayari imeshafuzu wakati Tunisia ikifuatia kwa pointi tatu, kila moja ikicheza mechi mbili.
Taifa Stars imevuna alama moja juzi baada ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Uganda katika Uwanja wa Al Medina, Rabat nchini humo.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Kaimu Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Muargentina Miguel Gamondi, amesema hivi sasa nguvu zao wanazielekeza katika mechi ya kesho kuhakikisha wanashinda.
Gamondi alisema lengo lao sasa ni kupata ushindi dhidi ya Tunisia kuhakikisha inatinga katika hatua ijayo.
Awali, kocha huyo alisema ukosefu wa umakini wa wachezaji wake ndiyo sababu ya kutopata ushindi katika mtanange dhidi ya Uganda.
Gamondi alisema timu yake ilikuwa ikipoteza mpira mara kwa mara uwanjani hasa kipindi cha kwanza hatua ambayo iliwapa makali wapinzani wake.
“Haya ni matokeo ya kusikitisha (1-1), mechi ilikuwa nzuri, tulikosa umiliki na Uganda walipoteza nafasi nyingi kuliko sisi, kipindi cha pili tulibadilika sana tulitengeza nafasi.
Soka ni mchezo wa makosa, tulitamani kushinda, lakini haikufanikiwa, tunaomba radhi kwa Watanzania,” alisema.
Nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta, alisema kila mchezaji lengo lake lilikuwa kupata ushindi dhidi ya Uganda lakini halikutumia hivyo sasa nguvu zao wanazihamishia dhidi ya Tunisia.
“Kila mmoja alikuwa anaona tunakwenda kupata pointi tatu, isivyo bahati tumepata pointi moja, wachezaji wameumia sana walienda kupambana kwa lengo la kupata ushindi lakini imetokea hivyo.
“Tunakwenda kuangalia kwa ukubwa mechi yetu dhidi ya Tunisia, mwalimu ameona makosa yetu hivyo tunakwenda kupambana tuone tunapataje pointi tatu,” alisema.




