RIYADH, Saudi Arabia
CRISTIANO Ronaldo amewasha moto baada ya kurejea katika timu ya Al-Nassr na kufunga bao pekee katika mchezo dhidi ya Al Fateh.
Pambano hilo la Ligi Kuu ya Saudi maarufu ‘Saudi Pro League’, lilipigwa katika Uwanja wa Maydan Tamweel Aloula uliopo mjini Al-Mubarraz, Al-Ahsa, Saudi Arabia.
Katika michuano hiyo,Al –Nassr ipo nafasi ya pili ikiwa na alama 52 baada ya kucheza mechi 21 huku vinara ikiwa Al-Hilal yenye pointi 53 baada ya kushuka dimbani mara 21 katika ligi hiyo.
Mchezaji huyo wa kimataifa kutoka Ureno, alifunga bao hilo katika dakika ya 18 ya pambano hilo ambapo Al Nassr ilishinda 2-0, bao la pili lilipachikwa wavuni na Aiman Yahya katika dakika ya 78 ya mchezo huo.
Awali, Nyota huyo wa Ureno alikosa mechi dhidi ya timu za Al Ittihad na Al Riyadh, mapema mwezi huu akipinga msaada wa kifedha kwa klabu hiyo katika dirisha la uhamisho la hivi majuzi.
Baada ya kupachika bao hilo, Ronaldo alionekana mtu mwenye kutabasamu kufuatia kurejea dimbani.
Mshambuliaji huyo wa zamani wa Man United katika pambano hilo, alifunga bao baada ya kupokea mpira kutoka kwa Sadio Mane, Ronaldo alijinyooshea kidole kisha akaelekeza chini akiashiria kwamba anabaki na klabu hiyo ya Saudia.
Furaha hiyo, imekuja baada ya kutokea sintofahamu kati ya klabu hiyo na Ronaldo ambaye alisema klabu yake inaonewa.
Hali hiyo, ilikuja baada ya wapinzani Al Hilal, kuwa na umiliki asilimia 75 ya wingi katika ligi hiyo ya Saudi Arabia.
Pia, Ronaldo alipinga usajili wa mchezaji mwenzake wa zamani wa Real Madrid, Karim Benzema kutoka Al Ittihad.
Hata hivyo, mgomo wake kwa Al-Nassr pia ni wa kwanza akiwa na umri wa miaka 41, Ronaldo analipwa kitita cha pauni 488,000 kwa siku nchini Saudi Arabia na ndiye mwanasoka anayelipwa fedha nyingi zaidi duniani hadi leo.
Mchezaji huyo katika mkataba wake, unajumuisha safari za ndege za kurudi, kukaa hoteli ya nyota tano kwa siku tano.
Kocha wa timu ya Taifa ya Ureno, Roberto Martinez alisisitiza kuwa Ronaldo ni mchezaji muhimu.
Aliiambia BBC Sport kuwa ni matarajio yake ya jinsi kazi inapaswa kufanywa na kujitolea kwa Ronaldo katika kila mchezo.
“Yeye ni mfungaji mabao, ni mchezaji muhimu kwetu, ni mchezaji ambaye sasa ni muhimu kwangu.
“Kama kocha wa timu ya taifa, mchezaji ambaye amefunga mabao 25 katika michezo 30 iliyopita ya kimataifa, sio kwamba anacheza kutokana na kile alichokifanya huko nyuma, ni kile ambacho anafanya sasa kuonesha uwezo wake,” alisema kocha huyo.
Ronaldo anashika nafasi ya tatu katika orodha ya wafungaji bora wa Ligi Kuu ya Saudia, amefunga mabao 18 katika michezo 17, lakini Ivan Toney anaongoza katika msimamo huo akiwa na mabao 20 katika mechi 20 alizocheza.




