Na AMINA KASHEBA
KOCHA Mkuu wa timu ya Simba,Steve Barker amekoleza moto wachezaji wake kwa kuwataka waweke akili yao katika michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano mingine.
Barker amesema hayo katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam,muda mfupi baada ya kumalizika mchezo kati ya Simba na Stade Malien.
Katika mchezo huo wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Simba ilishinda 1-0, tayari Wekundu wa Msimbazi wametolewa kwenye mashindano hayo.
“Nimefurahishwa na kiwango kizuri ambacho wachezaji wangu wamekionesha katika mechi hiyo.
“Pongezi kwa kucheza mchezo mzuri katika michuano hiyo ya kimataifa,hivi sasa michuano hii tumemaliza, tunarudi kupambana kusaka ubingwa wa ligi kuu,” alisema.
Barker alifafanua kuwa hivi sasa, wachezaji wake wanatakiwa kubadilisha mawazo yao na kuweka kichwani michezo ya ligi kuu na Kombe la FA.
“Tunapaswa kuwa imara na kuweka nguvu mpya ya kupambana katika ligi, lengo kubwa ni kufanya vizuri na kutimiza malengo tuliojiwekea ya kutwaa ubingwa na michuano ya FA,” alisema.
Hata hivyo, kocha huyo alisema ana imani wachezaji wake watafanya vizuri zaidi kwa vile wameanza kuelewa mfumo anaotaka wacheze.
Kwa upande wa mwakilishi wa wachezaji, Shomari Kapombe aliwashukuru viongozi wa Simba kwa jitihada kubwa walizozifanya katika timu hadi kufika hapo walipo.
“Natanguliza shukrani zetu kwa niaba ya wachezaji wenzangu kwa viongozi,mashabiki wetu, wamefanya mambo mengi makubwa, haikuwa matarajio yetu kama wachezaji kufikia hatua hii, imetokea bahati mbaya, tunaweza kusema ni matokeo ya mpira ambayo yanaweza kutokea muda wowote.
“Hili tumechukua kama funzo kwetu, tunakwenda kujiweka sawa katika msimu huu wa ligi, kikubwa nawaomba viongozi waendelee kuwa pamoja na sisi,tunatarajia kufanya vizuri katika ligiili m simu ujao turudi tena Ligi ya Mabingwa Afrika, msimu ujao,” alisema.
Kapombe aliwaomba viongozi wa klabu hiyo, kuendelea kuongeza nguvu zaidi katika timu ili ifanye vizuri.




