Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amewaagiza baadhi ya mawaziri alioambatana nao, wabaki mkoani Tanga kufuatilia masuala yaliyoibuliwa na wananchi na kuyatafutia ufumbuzi.
Masuala hayo, yalitokana na hoja zilizoibuliwa katika mikutano ya hadhara na wabunge wa mkoa wa Tanga na wananchi mbalimbali katika sekta za ardhi, mifugo, kilimo, maji, elimu na barabara.
Alitoa agizo hilo, akizungumza na wakazi wa Soni na Bumbuli katika mkutano wa hadhara uliofanyika stendi ya Soni, wilayani Lushoto, Mkoa wa Tanga.
Mapema, akijibu hoja kuhusu ubovu wa barabara wilayani Lushoto, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, alisema Rais Samia Suluhu Hassan, ametoa kibali cha kuanza ujenzi wa pande mbili barabara ya Soni – Bumbuli- Dindira hadi Old Korogwe.
“Barabara hii ilishatangazwa na sasa tunakamilisha taratibu za wakandarasi. Zikiwa tayari, mmoja ataanzia Soni kwa kujenga kilometa 22 na mwingine ataanzia Old Korogwe (KwaMeta hadi Kwa Shemsi) kwa kujenga kilometa 9.5,” alisema.
Alisema barabara ya sasa ya kutoka Mombo – Soni hadi Lushoto yenye urefu wa kilometa 32, imefanyiwa usanifu na inatafutiwa fedha ifanyiwe upanuzi.
Naye Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde, alisema Msajili wa Hazina, anamalizia uhakiki wa madeni ya zamani ya wakulima wa chai waliokuwa wanadai malipo katika kiwanda cha chai cha Mponde na kuongeza kuwa katika kipindi cha hivi karibuni hakuna madeni yoyote yaliyolimbikizwa.
Alisema kiwanda hicho ambacho kinahudumia Halmashauri mbili za Bumbuli na Korogwe, kinafanyiwa mpango wa kupata ‘line’ nyingine ya uzalishaji ili kupunguza mlundikano wa majani ya chai yaliyovunwa.
Alisema Bodi ya Chai imenunua kiwanda kingine Korogwe ambacho kinatarajiwa kuanza kazi kabla ya Juni, mwaka huu kisaidie kupunguza mzigo unaoenda kiwanda cha Mponde.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alikagua na kuzindua shule mpya ya sekondari ya amali ya Majulai iliyopo katika Kijiji cha Majulai, Kata ya Mwangoi, Tarafa ya Mlalo wilayani Lushoto.
Shule hiyo ambayo imejengwa kupitia mradi wa SEQUIP, tayari imesajiliwa, ina walimu sita na wanafunzi 89 ambao walianza masomo Januari 13, mwaka huu.
Akitoa taarifa ya ujenzi wa shule hiyo, Mkuu wa shule ya Sekondari Shita, ambayo ni shule mama, Mwalimu Ramadhani Mohammed, alisema mradi huo ambao umegharimu sh. milioni 584.28, ulianza kutekelezwa Oktoba 23, 2024 na hadi sasa, umetumia sh. milioni 581.81 na kwamba sh. milioni 2.46 zilizobakia ni za angalizo, kukamilisha ujenzi wa tenki na kulipa mafundi.




