Na AMINA KASHEBA
UNAWEZA kusema kitaeleweka leo,Yanga na Dodoma Jiji zitakapo pambana katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Pambano hilo, limepangwa kupigwa katika Uwanja wa KMC jijini Dar es Salaam kuanzia saa 1:00 usiku.
Katika msimamo wa ligi, Yanga ipo nafasi ya pili ikiwa na pointi 19 baada ya kushuka dimbani mara saba.
Timu ya Dodoma Jiji ipo nafasi ya 11 katika msimamo wa michuano hiyo, ikiwa na pointi 10 na imeshuka dimbani mara 10.
Akizungumza maandalizi ya mchezo huo, Kocha Msaidizi wa Yanga, Partick Mabedi alisema wamejipanga kuhakikisha wanapata ushindi ambao utawapa furaha mashabiki wa timu hiyo.
“Tunataka kurejesha nguvu yetu ya ushindi katika mchezo wa leo,pia maandalizi yako vizuri na wachezaji wana morali ya kutosha, wapo tayari kupambana kuhakikisha tunafanya vizuri,” alisema.
Mabedi alisema lengo lao katika mchezo wa leo ni kupata ushindi na kuirudisha heshima yao.
“Tunafahamu tutapata ushindani mkubwa kutoka wapinzani wetu nao wana wachezaji wengi wazuri,”alisema.
Mwakilishi wa wachezaji, Abubakari Ninju, alisema wachezaji wamejiandaa vizuri kuhakikisha wanapata ushindi katika mchezo wa leo, pia, kuwapa furaha mashabiki wa Yanga.
“Kwa niaba ya wachezaji tumejiandaa vizuri tupo fiti tutahakikisha tunacheza vizuri na kupata ushindi, tunatambua mchezo utakuwa mgumu, tumejiandaa kucheza katika kiwango kizuri ambacho kitatupa matokeo mazuri,” alisema.
Mchezaji huyo alisema wana amini watafanya vizuri mchezo wa leo kwa lengo la kuwapa furaha mashabiki zao.
Kocha wa Dodoma Jiji,Amani Josia alisema jukumu kubwa kama walimu ni kuwaweka tayari wachezaji wao katika utayari wa kusaka ushindi dhidi ya Yanga.
“Lengo la mechi hii ni kuwapa furaha mashabiki zetu, ipo namna ya kupambana kuhakikisha tunapata ushindi katika mechi kama hizi kwasababu ya aina ya timu tunayoenda kukutana nao kuwa na wachezaji wengi wazuri wenye uzoefu mkubwa,” alisema.
Kocha huyo alisema wanaenda kukutana na Yanga, ambayo imetoka kupoteza mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi, Al Ahly.
“Yanga ina wachezaji wazuri hata kama wasipocheza waliocheza mechi na Al Ahly, bado wako vizuri tutacheza kutokana na kiwango chetu lengo ni kupata ushindi na kuondoka Dar es Salaam tukiwa na pointi tatu,” alisema.
Mwishoni mwa wiki, Yanga ilichapwa mabao 2-0 na Al Ahly katika pambano lililopigwa nchini Misri.
Timu hizo zinatarajiwa kupambana Januari 31,visiwani Zanzibar, ambapo maandalizi kuelekea pambano hilo yanaendelea kufanyika.




