Na AMINA KASHEBA
MENEJA wa Habari na Mawasiliano wa klabu ya Simba, Ahmed Ally amewatuliza mashabiki, wanachama wa klabu hiyo na kuwataka waache kutoa lawama kwa viongozi badala yake wawape sapoti.
Ally alisema hayo Dar es Salaam,jana, kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha wanachama wa timu hiyo wana shikamana na viongozi, timu ifanye vizuri katika mashindano yote yanayowakabili.
“Tumekuwa tunafanya vizuri misimu minane nyuma, kutokana na kuwepo umoja, tumekuwa na historia hiyo kucheza robo fainali saba za Bara la Afrika, kama itatokea tukashindwa basi mashabiki wanatakiwa kuacha kutoa lawama kwa viongozi na kuendelea kuisapoti.
“Hata kama tutachekwa na wapinzani wetu, lakini wanachama wa Simba wanatakiwa kutowalaumu viongozi wetu kwa sababu huu ni mpira,” alisema.
Meneja huyo aliongeza kwamba, viongozi hao ndiyo walisababisha timu yao ikafanya vizuri.
“Hao wanao tucheka, mwaka jana walishindwa kufanya vizuri katika mshindano ya msimu uliopita na kuishia njiani.
“Tuna uwezo wa kufanya vizuri katika michezo mitatu iliyobaki ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), “alisema.
Hata hivyo, Meneja huyo alisisitiza kwamba Simba ina nafasi ya kufanya vizuri katika michezo mitatu iliyobaki ya michuano (CAFCL).
Wiki iliyopita Simba ilipoteza mchezo wake wa tatu kwa kufungwa bao 1-0 na Esperance Tunis ya Tunisia.
Timu hizo zinatarajiwa kucheza tena Januari 31, mwaka huu katika Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, Ally aliwaomba mashabiki, wanachama wa klabu hiyo kuwa kitu kimoja ana imani upepo huo mbaya utaondoka ndani ya klabu na kufanya vizuri kama ilivyokuwa siku za nyuma.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, Crescentius Magori alisema mashabiki wa timu hiyo wanatakiwa kutokata tamaa kwa vile Simba bado ina nafasi ya kufanya vizuri.
“Bado Simba ina nafasi ya kufanya vizuri katika michezo mitatu iliyobaki, hivi sasa mashabiki wasiiache timu bado nafasi ya kufanya vizuri ipo,” alisema Magori.




