Na NASRA KITANA
BAADA ya Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars, Miguel Gamondi, kutia saini mkataba wa kuinoa timu hiyo, wadau wa soka nchini wameibuka na kusema anapaswa kupewa ushirikiano wa kutosha kufikia malengo, hususan katika mashindano ya Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON 2027).
Gamondi alitia saini mkataba wa kuinoa timu hiyo kwa kipindi cha miaka miwili.
Wakizungumza na UHURU kwa nyakati tofauti, Dar es Salaam, jana aliyekuwa Kocha wa timu ya Taifa Stars, Charles Mkwasa, Kennedy Mwaisabula na Boniface Pawasa walisema hiyo ni hatua kubwa kwa serikali na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania(TFF) kumbakisha Gamondi ndani ya kikosi hicho, kwa kuwa ana uwezo mkubwa wa kuifundisha timu hiyo.
Mkwasa alisema Gamondi analijua vizuri soka la Tanzania na wachezaji wake wote, hivyo itakuwa rahisi kujenga kikosi imara cha ushindani.
Kocha huyo alisisitiza kitu kinachotakiwa kufanywa hivi sasa ni kuhakikisha timu inaingia kambini mapema na kufanya maandalizi ya kutosha, ifanye vizuri kila mchezo.
“Ninawapongeza kwa kuendelea kumuamini Gamondi, ni kocha mwenye mafanikio makubwa ninaamini atajenga kikosi kilicho bora kwa vile anawafahamu wachezaji wengi,” alisema.
Mkwasa alisema Watanzania wanatakiwa kumuunga mkono Gamondi, atimize majukumu yake vizuri.
Kwa upande wake, Mchambuzi wa soka nchini, Mwaisabula aliwapongeza viongozi wa serikali na TFF kwa kuendelea kuziandaa vyema timu zote za taifa.
“Watu wanapaswa kutambua kuwa, mashabiki wana mchango mkubwa katika timu kufanya vizuri, hivyo tunatakiwa kumpa ushirikiano wa kutosha kocha wetu kuanzia mwanzo wa mashindano hadi mwisho, kwa kuwa hiyo ni silaha yetu ya mafanikio,” alisema Mwaisabula.
Kiongozi huyo alieleza Watanzania siku zote wanataka ushindi, hivyo jambo ambalo wanapaswa kufahamu ni kwamba, siyo kila wakati timu itashinda.
Alisema kinachotakiwa ni kukubaliana na matokeo yeyote na kuwa bega kwa bega na kocha na wachezaji wake.
Naye, aliyekuwa mchezaji wa zamani wa Simba na timu ya Taifa, Pawasa alisema wachezaji wanatakiwa kupambana kwa nguvu zote.
“Tunajua mashindano ya AFCON yanafanyika nchini kwetu, Kenya na Uganda, hivyo kama nchi mwenyeji tunatakiwa kupambana kufikia malengo tuliojiwekea. Mwalimu aangalie wapi kuna upungufu na kurekebisha mapema, kabla ya kuanza kwa mashindano,” alisema Pawasa.
AFCON 2027 inatarajiwa kufanyika kuanzia Julai, mwakani kwa ushirikiano wa Tanzania, Kenya na Uganda.




