Na NASRA KITANA
KUFUATIA ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars, Kocha wa Simba, Steve Barker amesema kuwa ushindi huo umewaongezea morali na kasi ya kupambana katika mchezo unaofuata.
Simba, iliibuka kidedea kwa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida BS katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Uwanja wa Airtel uliopo mkoani Singida.
Baada ya mchezo huo Simba imefunga safari kuelekea Arusha kwa ajili ya mchezo wake mwingine dhidi ya TRA utakaochezwa kesho katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha.
Akizungumza mara baada ya mchezo huo, Kocha Barker alisema kuwa ilikuwa mechi ngumu kwao kwani walicheza uwanja wa ugenini, lakini wachezaji wake walipambana kuhakikisha wanafikia malengo ya kupata ushindi.
Alisisitiza, ushindi huo umewaongezea morali na kasi ya kupambana kuhakikisha wanaendelea kufanya vyema katika mechi zitakazofuata za michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Alisema amefurahia matokeo hayo na kwamba anawapongeza wachezaji wote kwani kila mmoja alitimiza majukumu yake uwanjani na kuhakikisha wanaibuka kidedea.
Alisema bado anahitaji wachezaji wake kutumia vyema nafasi ambazo wanazipata ili kuweza kushinda mabao mengi katika kila mchezo.
“Ujue mchezo huo umetuongezea morari ya kutosha kuelekea katika mechi zinazofuata hasa dhidi ya TRA, hivyo hatuna muda wa kupumzika tutapambana kuhakikisha tunafanya maandalizi kwa ajili ya mchezo wetu huo, lengo likiwa ni kupata ushindi na kujizolea pointi tatu muhimu,” alisema Barker.
Kocha huyo alisema kulikuwa na makosa ambayo wachezaji wake waliyafanya katika mchezo uliopita, hivyo ameyafanyia kazi katika uwanja wa mazoezi na kwamba ana imani watapata ushindi mechi inayofuata.
Alisema hana hofu na kikosi alichokuwa nacho kwani kila mchezaji amekuwa akijituma na kuonesha uwezo mkubwa kuhakikisha anaisaidia timu kufanya vyema.
Naye Kocha wa Singida BS, David Ouma alisema kuwa timu yao ilipoteza mechi hiyo baada ya kuzidiwa mbinu na wachezaji wa Simba.
Alisema timu yake ilicheza vizuri na kuonesha kiwango kikubwa tofauti na wapinzani wao lakini bahati haikuwa yao baada ya kuzidiwa mbinu, hivyo watahakikisha wanakwenda kufanyia marekebisho katika mapungufu yaliyojitokeza ili kupata ushindi katika mechi zijazo.
“Timu bora imepoteza katika mchezo wetu jambo ambalo limeniumiza japokuwa wachezaji wangu walicheza katika kiwango kizuri, ninajua tuna mechi nyingi mbele yetu tutapambana mwanzo hadi mwisho kuweza kupata ushindi na kujihakikishia nafasi nzuri katika msimamo wa ligi,” alisema Ouma.
Kocha huyo alisema kuwa kwa hivi sasa wanakwenda kujipanga kwa ajili ya mchezo unaofuata dhidi ya Mbeya City na lengo lao ni kuhakikisha wanapata ushindi.
Katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba inashika nafasi ya nne ikiwa na pointi 27 baada ya kushuka dimbani mara 12 huku Singida BS ikishika nafasi ya 10 kwa pointi 19 baada ya kushuka dimbani mara 13.




