Na FRED ALFRED, Dodoma
SERIKALI imetenga sh. bilioni 240 kwa ujenzi wa masoko 30 ya kisasa yenye hadhi ya mkoa nchini.
Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuboresha mazingira ya biashara, kuongeza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.
Hayo yalibainishwa jijini hapa na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, alipotembelea Soko la Machinga.
Msigwa ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alisema pamoja na ujenzi wa masoko makubwa, itaendelea kujenga mengine madogo katika maeneo mbalimbali ya miji na vituo vya biashara.
Pia, kuwapa wafanyabiashara wadogo, hususan wamachinga maeneo salama na rafiki ya kufanyia shughuli zao.
“Serikali itaendelea kujenga masoko madogo katika maeneo ya katikati ya miji kurahisisha mazingira ya wamachinga kufanya biashara zao kwa utulivu na usalama,” alisema.
Pia, serikali imetenga sh. bilioni 264 za ujenzi wa stendi 32 za kisasa katika maeneo yenye muunganiko mkubwa wa usafiri na biashara, utekelezaji wake ukiwa umefikia zaidi ya asilimia 80.
Akizungumzia Soko la Machinga la Dodoma, Msigwa alisema awali lilipangwa kuwahudumia wafanyabiashara 2,700, hivi sasa lina wapo zaidi ya 4,800, jambo linaloonesha mafanikio ya mpango wa serikali wa kujenga masoko ya kisasa kwa vijana na wafanyabiashara wadogo.
Msigwa alisema takribani asilimia 80 ya wafanyabiashara wanaofanya shughuli zao katika soko hilo ni vijana, hali inayodhihirisha masoko hayo yamekuwa chanzo muhimu cha ajira na kipato.
“Soko hili ni miongoni mwa masoko 15 yanayojengwa na serikali nchini. Masoko 10 tayari yamekamilika kwa asilimia 100 na ujenzi wa masoko matano unaendelea.
“Dhamira ya serikali ni kuendelea kutengeneza mazingira bora ya kufanyia biashara,” alisema.
Aliendelea kusema, masoko hayo yamejengwa kwa gharama ya zaidi ya sh. bilioni 15 na Soko la Machinga la Dodoma pekee, hupokea zaidi ya watu 10,000 kwa siku wanaofika kununua bidhaa.
Aliwataka vijana kutumia fursa zinazotolewa na serikali kupitia masoko hayo kujiongezea kipato na kujiepusha na vitendo vya uhalifu.
KUHUSU MIKUTANO YA HADHARA
Msigwa alisema serikali itaruhusu tena kufanyika mikutano ya hadhara, baada ya vyombo vya ulinzi na usalama, kujiridhisha kama hali inaruhusu.
Alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu masuala mbalimbali ya utekelezaji wa shughuli za serikali.
Alisema uamuzi wa kuruhusu mikutano ya hadhara, utategemea tathmini ya vyombo vya ulinzi na usalama, ambavyo vina wajibu wa kuhakikisha amani na utulivu vinakuwepo nchini.
Alisisitiza kuwa, suala la ulinzi na usalama halina mbadala.
Alieleza kuwa, serikali imepokea taarifa za kuwepo baadhi ya watu wenye nia ovu wanaoweza kutumia mikutano ya hadhara kufanya vitendo vitakavyohatarisha usalama wa nchi.
“Ni jukumu la serikali kuhakikisha inalinda wananchi na mali zao,”alisema.
Msigwa alisema kazi ya vyombo vya ulinzi na usalama ni kuzuia vitendo vya uhalifu kabla havijatokea.
Alisema vikibaini hakuna tena viashiria vya vitendo vyenye nia ovu, mikutano ya hadhara itaruhusiwa kuendelea kama kawaida.
Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kudumisha amani.




