Na SELINA MATHEW, DODOMA
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametoa maagizo manne kwa wizara na wadau wa sekta ya mawasiliano nchini, huku ikiwamo kuondoa urasimu unaochelewesha utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya mawasiliano.
Pia, ameitaka sekta binafsi kutoa ushirikiano mpana kuhakikisha hakuna Mtanzania anayebaki nyuma katika safari ya uchumi wa kidigitali.
Dk. Samia aliyasema hayo jijini hapa alipokuwa akizindua minara 758, maunganisho ya mkondo wa mawasiliano katika wilaya 85 na kukabidhi mkongo wa mawasiliano serikalini.
Aliupongeza Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), kwa kufikisha huduma za mawasiliano hadi visiwani na maeneo ya pembezoni na kwamba hatua hiyo inaakisi Tanzania inayotaka kuona maendeleo jumuishi.
Alisisitiza kuwa mawasiliano ni daraja la fursa kwa wananchi wote na nyenzo muhimu ya uwekezaji, ajira na ustawi wa jamii, hivyo wadau wanapaswa kuendeleza ubunifu, kukuza uwekezaji na kutanua miundombinu kuendana na kasi ya dunia ya sasa.
Vilevile, Rais Samia alibainisha kuwa maendeleo ya sekta ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), yanachochea ajira na kuongeza tija katika uzalishaji, jambo linalochangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi na maendeleo ya kijamii.
Alisema serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika miundombinu ya mawasiliano, hususani mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, ambao umefikia kilometa 15,167, ukiunganisha mikoa yote ya Tanzania Bara pamoja na wilaya 121 kati ya 139, ikilinganishwa na wilaya 36 pekee mwaka 2021.
Aidha, mkongo huo umeunganisha nchi jirani za Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Zambia, Malawi na Msumbiji, huku hatua za kuunganisha Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) zikiendelea.
Kutokana na uwekezaji huo, alisema Tanzania imekuwa kitovu muhimu cha mawasiliano katika ukanda huo, ambapo hadi sasa laini za simu zimefikia milioni 106.9 na watumiaji wa intaneti milioni 58.1, huku matumizi ya simu janja yakifikia asilimia 41.84.
Mbali na hilo alisema kukamilika kwa ujenzi wa minara hiyo 758 ya mawasiliano kumeongeza upatikanaji wa huduma kwa zaidi ya wananchi milioni 8.5, hasa katika maeneo ya vijijini na mipakani.
Alisema hatua hiyo imeondoa changamoto ya wananchi kutumia mitandao ya mawasiliano ya nchi jirani na badala yake kuwajumuisha kikamilifu katika mfumo wa mawasiliano wa taifa.
“Zamani simu ilikuwa anasa, leo ni hitaji muhimu kwa uchumi wa kisasa. Mawasiliano siyo tena anasa bali ni uti wa mgongo wa uchumi,” alisisitiza.
Akemea urasimu
Rais Samia aliziagiza halmashauri zote nchini kuondoa urasimu katika utoaji wa vibali vya miradi ya mawasiliano kuepusha upotevu wa muda na fedha.
Alisema wakuu wa mikoa wanapaswa kuwasimamia wakuu wa wilaya kuhakikisha vibali vinatolewa kwa wakati miradi itekelezwe kama ilivyopangwa.
MAELEKEZO MAHSUSI
Dk. Samia aliiagiza Wizara kushirikiana na Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana pamoja na wadau wa sekta hiyo, kuhakikisha vijana wananufaika ipasavyo na huduma za mkongo wa taifa wa mawasiliano hususani kuchochea kukuza ubunifu wa kidigiti na kuongeza fursa za ajira na uchumi.
Agizo la pili, alisema katika hatua ya kutekeleza agizo la kimataifa la kutomwacha mtu nyuma katika maendeleo, wizara husika iratibu na kuhakikisha wilaya zote ambazo bado hazijafikiwa na huduma za mkongo, kazi inafanyika kisha wajipange ngazi za chini za kata na vitongoji.
“Jambo hili lina manufaa makubwa kwa sababu wakati mwingine tunapokuwa na vikao vya dharura na ngazi za chini tunatumia mfumo wa kuwasiliana kwa kutumia mfumo huu, tunafanya mikutano yetu tunakubalina na tunamaliza vizuri. Yote kwa sababu mkongo umefika kule chini,” alisema.
Alibainisha kuwa msisitizo huo, utawezesha wananchi wote kunufaika na huduma za mawasiliano na fursa zitokanazo na uchumi wa kidigiti.
Tatu, aliagiza waliokabidhiwa dhamana kuhakikisha miundombinu ya mkongo wa taifa wa mawasiliano inalindwa na kutunzwa vyema kwa kuwa ni mhimili wa uchumi na ustawi wa nchi, ulinzi na usalama wa taifa.
Nne, aliagiza huduma za mawasialiano zinazotolewa nchini zizingatie maadili, mila na utamaduni wa kitanzania kwa kuwa hali hiyo, isipodhibitiwa nchi itaishia kuwa na kizazi kisicho na maadili na uzalendo kwa taifa.
“Nimetembelea banda la Huawei wamesema watatengeneza mfumo wa AI wa Kiswahili kwa Watanzania, utakaolinda maadili ya Watanzania, nikuombe Waziri shirikiana nao kwa karibu ili wakamilishe hili mapema. vijana wakiupata kiwango cha ubunifu kitakuwa zaidi.
“Kuna vijana hawajawahi kusoma kompyuta lakini anafanya kazi zake ndani yake huwezi kuamini, kamilisheni hili mapema,”alisisitiza.
Vilevile, aliiagiza Wizara ya Mawasiliano kushirikiana na Kampuni ya Huawei kuendeleza mfumo wa akili bandia (AI) kwa Kiswahili utakaolinda maadili ya Watanzania na kuchochea ubunifu kwa vijana.
Alisisitiza juhudi hizo zote zinalenga kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2025-2030 inayolenga kujenga uchumi shindani unaoongozwa na maarifa, teknolojia na ubunifu.
“Uwekezaji huo unaweka msingi imara wa Tanzania ya kidigitali yenye huduma bora za mawasiliano na nyenzo za kukuza tija kwa wananchi, itakayomudu ushindani wa kimataifa ikiwemo kujenga uchumi imara wa taifa,” alisema.
SALAMU ZA VIONGOZI
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angellah Kairuki, alisema tayari wizara imashasaini mikataba ya ujenzi wa minara 201 itakayotekelezwa katika vijiji 263 na kata 201, ambayo itakamilika mwaka 2027 na kunufaisha takribani wananchi milioni 2.8.
Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mohammed Abdulla, alisema lengo lililopo ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 hakuna eneo litakalokuwa halijafikiwa na huduma za mawasiliano nchini.
Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Mhandisi Peter Mwasalyanda, alisema kwa mujibu wa UCSAF, mradi wa ujenzi wa minara 758 na uboreshaji wa minara 304 umegharimu sh. bilioni 126 na kwamba sh. bilioni 55 ni mkopo kutoka Benki ya Dunia na sh. bilioni 71 ni fedha za ndani.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL), Moremi Marwa, alisema mradi wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ulioanza kutekelezwa kwa awamu mbalimbali kuanzia 2009 hadi sasa umefikisha huduma katika wilaya 121 kati ya 139 za Tanzania Bara sawa na asilimia 82.
Pia, alisema kwa sasa wanaendelea katika wilaya 18, wamefikia wilaya zote Tanzania Bara na hadi Aprili 2027 watamalizia nchi jirani ya DRC.




