Na Hamis Shimye
TEKNOLOJIA imekuwa nyenzo muhimu inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii duniani, kutokana na uwezo wake wa kurahisisha maisha ya binadamu na kuongeza ufanisi katika shughuli mbalimbali.
Teknolojia inaelezwa kama sehemu muhimu ya matumizi ya maarifa ya kisayansi na ujuzi katika kubuni na kutumia vifaa au mifumo inayosaidia kutatua matatizo ya kila siku.
Wataalamu wanasema teknolojia imegawanyika katika aina mbalimbali zikiwemo teknolojia ya kidijitali kama simu na kompyuta, teknolojia ya mawasiliano kama intaneti na televisheni, teknolojia ya kilimo inayoboresha uzalishaji, pamoja na teknolojia ya afya na nishati.
Umuhimu huo, umesababisha China kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kiteknolojia na Tanzania katika juhudi za kuchochea maendeleo ya uchumi wa kidijitali na kupunguza pengo la huduma kati ya mijini na vijijini.
Maonesho ya Teknolojia ya Juu ya China yaliyofanyika katika Kituo cha Biashara na Usafirishaji, Dar es Salaam yamekuwa na shabaha kubwa kwa kampuni za China kuonyesha teknolojia pamoja na kuwapa nafasi viongozi na wadau wa sekta ya teknolojia kujadili fursa za ushirikiano wa ubunifu.
WAZIRI KAIRUKI
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Teknolojia na Mawasiliano, Angellah Kairuki, alisema ushirikiano kati ya Tanzania na China umebadilika kwa kiwango kikubwa katika kipindi cha muongo mmoja uliopita, kutoka miradi ya miundombinu hadi kufikia matumizi ya teknolojia za kisasa.
Alisema maeneo ambayo tayari yameanza kunufaisha wananchi ni pamoja na matumizi ya akili bandia (AI) katika huduma za afya, upanuzi wa mawasiliano vijijini, mifumo ya nishati jadidifu kama sola, pamoja na maendeleo ya kilimo cha kisasa kinachotumia teknolojia.
“Teknolojia hizi zimekuwa chachu ya fursa mpya kwa wakulima na wafanyabiashara wadogo, huku zikiboresha upatikanaji wa huduma muhimu kama elimu na afya,” alisema Kairuki.
Aidha, alibainisha kuwa matumizi ya majukwaa ya elimu ya mtandaoni na uchunguzi wa magonjwa kwa kutumia AI yameanza kupunguza tofauti ya huduma kati ya maeneo ya mijini na vijijini.
Katika sekta ya nishati, Kairuki alisema teknolojia za kijani kama mifumo ya sola na uhifadhi wa nishati zimeiwezesha Tanzania kuongeza upatikanaji wa umeme katika shule, vituo vya afya na shughuli za kilimo.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa maonesho ya teknolojia lazima yaletwe katika matokeo halisi kwa kuimarisha ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi, pamoja na kuweka vivutio vya uwekezaji vitakavyoharakisha upatikanaji wa teknolojia nchini.
Pia, alitoa wito wa kuwekeza zaidi katika uhamishaji wa teknolojia na mafunzo kwa vitendo kupitia vituo vya pamoja vya mafunzo, ili kuwawezesha wahandisi, mafundi na wajasiriamali wa Kitanzania kushiriki kikamilifu katika ubunifu na maendeleo ya teknolojia.
“Tunahitaji ubunifu wa kijani unaoleta matokeo yanayopimika, ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa vijiji vilivyounganishwa kidijitali na kuboreshwa kwa maisha ya wananchi,” alisisitiza.
BALOZI WA CHINA AZUNGUMZA
Kwa upande wake, Balozi wa China nchini Tanzania, Chen Mingjian alisema maonyesho hayo ni safari bora ya ushirikiano wa kiteknolojia katika kukuza uchumi wa kidijitali nchini Tanzania.
Alisema Ufunguzi wa Maonesho ya Kiteknolojia “Experience China” High-Tech Fair ni dhamira kubwa ya China kuhakikisha mafanikio hayo yanakuwa sehemu ya mabadiliko nchini Tanzania.
Balozi Chen alisema maonyesho hayo yameangazia kila kitu kuanzia roboti za kuvutia, teknolojia ya hali ya juu kama vile miwani mahiri ya AI, ndege zisizo na rubani kubwa za kilimo, na mifumo ya kaya ya umeme wa jua.
“Tunaishukuru Tanzania pamoja na Waziri Anjela Kairuki kushiriki maonesho hayo. Tutarajie ushirikiano zaidi kati ya China na Tanzania katika uvumbuzi wa kisayansi na kiteknolojia” alisema
Aidha, alisema China itaendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania katika kuendeleza sekta ya teknolojia na kuhakikisha maendeleo ya kidijitali yanawafikia wananchi wengi zaidi.
“Ushirikiano huo unatarajiwa kuimarisha zaidi nafasi ya Tanzania katika uchumi wa kidijitali barani Afrika na kuleta maendeleo endelevu katika sekta mbalimbali muhimu.” Alisema
Faida za Maonesho ya Teknolojia ya Juu ya China kwa Tanzania
Maonesho haya yana manufaa kadhaa kwa Tanzania kupitia ushirikiano wake na China, hususan katika kukuza uchumi wa kidijitali na ubunifu wa teknolojia. Faida kuu ni pamoja na Kukuza uchumi wa kidijitali.
Hii itasaidia kuharakisha matumizi ya teknolojia kama AI, mifumo ya kidijitali na huduma za mtandaoni katika sekta mbalimbali za uchumi.
Pia, itasaidia kuvutia uwekezaji mpya
Maonesho hufungua milango kwa wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza katika sekta za teknolojia, nishati na mawasiliano.
Aidha, maonesho haya yatasaidia kuhamasisha ubunifu wa ndani, wabunifu na wajasiriamali wa Kitanzania wanapata nafasi ya kujifunza teknolojia mpya na kuibua suluhisho zinazofaa mazingira ya nchini.
Kuboresha huduma za kijamii. Teknolojia zinazooneshwa kama AI katika afya na majukwaa ya elimu ya mtandaoni husaidia kuboresha upatikanaji wa huduma vijijini na mijini.
Faida nyingine ni kupunguza pengo la mijini na vijijini. Upanuzi wa mawasiliano na teknolojia za kidijitali unasaidia vijiji kupata huduma ambazo awali zilipatikana mijini pekee.
Kujenga ujuzi na maarifa. Kupitia mafunzo na ushirikiano wa kiufundi, wataalamu wa Tanzania hupata ujuzi mpya wa teknolojia za kisasa.
Hivyo, maonesho haya ni jukwaa muhimu la kuharakisha maendeleo ya kiteknolojia na kiuchumi nchini, huku yakiongeza ushirikiano wa kimkakati kati ya Tanzania na China.



