Na MWANDISHI MAALUMU, Njombe
TIMU ya netiboli ya Ofisi ya Makamu wa Rais, inatarajia kufungua pazia la Michezo ya Mei Mosi kwa kuumana na kikosi cha Wizara ya Maji Aprili 16, 2026.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Kamati ya Mashindano ya Mei Mosi Taifa, jana, mtanange huo utafanyika katika Uwanja wa Mji Mwema mjini Njombe ukiwa ni sehemu ya shamrashamra ya maadhimisho ya Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani, ambayo kitaifa yanafanyika mkoani humo.
Akizungumzia mashindano hayo, Katibu wa Klabu ya Michezo Ofisi ya Makamu wa Rais, Marwa Nyaisawa, alisema timu yao imejiandaa vyema kutoa ushindani katika michezo hiyo.
“Tunatambua ni mara yetu ya kwanza kushiriki michezo hii kupitia timu ya mpira wa pete (netiboli) lakini kwa maandalizi tuliyofanya tunatarajia kutoa ushindani kuanzia hatua ya makundi na kuendelea,” alisema Nyaisawa.
Alisema wanatambua ugumu wa michezo ya Mei Mosi kutokana na kila timu kufanya maandalizi makubwa, hata hivyo wamedhamiria kuibuka washindi bila kujali ubora wa washiriki wengine.
“Benchi letu la ufundi la limeweza kujenga morali na hali ya kujiamini kwa wachezaji, kwa hiyo tunaamini tutaingia katika mashindano tukiwa fiti kuonesha ushindani,” alitamba.
Alisifu ratiba ya michezo hiyo kupangwa vizuri ambapo katika hatua ya makundi, timu ya Ofisi ya Makamu wa Rais imepangwa Kundi H pamoja na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Wizara ya Maji na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.
Katibu huyo alieleza baada ya mchezo dhidi ya Wizara ya Maji, Aprili 17 watavaana na timu ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma na mechi ya mwisho ya hatua ya makundi itakuwa dhidi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Aprili 18.
Kwa upande wake, Kocha wa timu ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mafuru Buriro alisema kikosi chake kipo tayari kwa michezo hiyo ambayo wataitumia kusuka kikosi imara kinachotarajia kutoa ushindani katika mashindano mengine ya kitaifa ya netiboli.
“Wachezaji wote wapo tayari na tunazidi kuimarika siku hadi siku na benchi la ufundi linafanyia kazi kasoro tunazoziona katika uwanja wa mazoezi na tumekusudia kuonesha kitu tofauti kwa wapinzani wetu katika michezo hii,” alisema Buriro.
Kaulimbiu ya Michezo ya Mei Mosi, 2026 inasema: “Michezo kwa Afya, Ajira, Furaha na Kazi Inaendelea; Kazi zenye staha ni Nguzo Imara kwa Maendeleo Endelevu katika Utekelezaji wa Dira 2050”.




