Na MWANDISHI WETU
RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan ametoa agizo lingine kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, mamlaka zote zinazohusika na michezo, kuhakikisha zinaiandaa mapema timu ya wavulana wenye umri chini ya miaka 17 ‘Serengeti Boys’.
Agizo hilo limetolewa ikiwa ni wiki moja baada ya kutoa agio kama hilo kwa mamlaka husika, kufanya maandalizi ya mapema kwa timu ya wanawake wenye umri chini ya miaka 20 ‘Serengeti Girls’ iliyofuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia.
Juzi, Serengeti Boys ilifuzu fainali za Kombe la Dunia 2026, zitakazofanyika Disemba, mwaka huu nchini Qatar.
Serengeti Boys ilikata tiketi ya kucheza fainali hizo baada ya kuifunga Angola mabao 3-0, katika pambano lililopigwa Uwanja wa Mohammed VI football Academy Pitch11, nchini Morocco.
Katika mchezo huo, Tanzania ambayo ipo kundi C, ikiwa na Msumbiji, Angola na Mali, ilipata mabao ya ushindi kupitia Razaki Juma dakika ya 28 , Hassani Kizinga alifunga bao la pili dakika ya 52 huku bao la tatu likipachikwa wavuni na Sadam Hussein dakika ya 68.
Taarifa iliyowekwa katika ukurasa wa Instagram wa Rais Samia, wenye wafuasi zaidi ya milioni tatu, Rais Samia alisema anaipongeza timu hiyo kwa kufuzu Kombe la Dunia.
Rais Samia alisema kufuzu kwa timu hiyo kumeonesha wazi uwezo, juhudi na nidhamu ya vijana wa Tanzania katika kuiwakilisha, kuipeperusha vyema bendera ya nchi katika anga la kimataifa.
“Ninaipongeza Serengeti Boys kwa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia mwaka 2026, mafanikio haya ni fahari kubwa kwa taifa letu na ni ushahidi wa vipaji, juhudi na nidhamu ya vijana wetu katika kuipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa,” alieleza Rais Samia.
Aidha, Rais Samia ameitakia kila la kheri timu hiyo ya vijana katika maandalizi ya mashindano.
Rais Dk. Samia aliihakikishia timu hiyo ushirikiano na maandalizi bora kutoka serikalini.




