Na MWANDISHI WETU
WAKAGUZI kutoka Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF), Lakshmikanth Karunanithi na Eduard Captan, wameeleza kuridhishwa na maendeleo ya maboresho ya miundombinu ya viwanja vinavyotarajiwa kutumika katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) baada ya kufanya ukaguzi wa maeneo mbalimbali yanayoandaliwa kwa ajili ya mashindano hayo.
Katika ziara hiyo, wakaguzi hao wametembelea Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam na kukagua maendeleo ya maboresho ya sehemu ya kuchezea ,maeneo maalumu ya wageni na viongozi mashuhuri (VVIP), pamoja na sehemu zitakazotumika na wanahabari wakati wa mashindano.
Aidha,wametembelea viwanja vya mazoezi vya Gymkhana II na Faras vinavyoandaliwa kuhudumia timu zitakazoshiriki AFCON 2027. Wakaguzi hao walipata fursa ya kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji wa maboresho yanayoendelea katika viwanja hivyo.
Baada ya ukaguzi huo, wakaguzi wa CAF wamebainisha kuwa kasi ya utekelezaji wa maboresho pamoja na maendeleo ya ujenzi wa miundombinu hiyo yanaonesha dhamira ya kuhakikisha viwanja vinakidhi viwango vinavyohitajika kwa ajili ya mashindano hayo makubwa ya soka barani Afrika.
Vilevile,Ukaguzi huo ni sehemu ya tathmini ya mara kwa mara inayofanywa na CAF kufuatilia maandalizi ya nchi mwenyeji kuelekea AFCON 2027 na kuhakikisha miundombinu yote inakamilika kwa ubora na kwa wakati.




