Na MWANDISHI WETU
KUFUATIA ushindi mnono wa mabao 11-0 dhidi ya Djibouti, Kocha wa timu ya taifa ya Vijana Chini ya Umri wa Miaka 17, ‘Serengeti Boys’, Elieneza Nsanganzelu amesema amefurahishwa na kiwango walichoonyesha wachezaji wake.
Serengeti Boys, iliibuka na ushindi wa mabao 11-0 mbele ya Djibouti, katika mchezo wa kufuzu kucheza michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (AFCON 2026), Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), katika mchezo uliofanyika Uwanja wa Diredawa nchini Ethiopia.
Katika pambano la kwanza, Serengeti Boys iliibuka na ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Sudan, mechi iliyofanyika nchini humo.
Akizungumza mara baada ya mchezo huo juzi, kocha Nsanganzelu alisema amefurahishwa na kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji wake na kwamba ana imani wataendelea kufanya vyema na kufikia malengo ya kufuzu michuano hiyo.
“Ninawapongeza wachezaji wangu kwa kuonyesha kiwango bora zaidi ikiwemo kufunga mabo mengi tofauti na awali.
“Kila mchezaji alitimiza majukumu yake na kuhakikisha timu inapata ushindi kwani malengo yetu ni kufanya vizuri na kufuzu michuano hiyo msimu huu,” alisema.
Nsanganzelu alisema walikutana na timu ngumu, lakini walifanikiwa kupata ushindi mnono kutokana na kufanya maandalizi ya kutosha kabla ya kuanza michuano.
Alisema kila mchezaji alitimiza majukumu yake katika mchezo huo na kuhakikisha wanafikia malengo ya kupata ushindi mnono.
“Tumekuwa na kikosi bora kutokana na kukiandaa kwa kipindi cha mwaka mzima, hii ni faida kwetu na malengo ni kuendelea kufanya vizuri zaidi katika mechi zitakazofuata,” alisema.
Kwa upande wake mchezaji wa Serengeti Boys, Luqman Ally, alisema alifanikiwa kupachika mabao sita peke yake kutokana na ushirikiano alioupata kutoka kwa wachezaji wenzake.
“Kikubwa kilichonifanya kufunga mabao sita ni kujituma na wachezaji wote walitoa ushirikiano mzuri kwangu.
“Tunakwenda kucheza na Uganda ambayo siyo timu nyepesi, lakini tunawaahidi Watanzania kwamba tutapambana kuhakikisha tunapata matokeo mazuri,” alisema.
Mabao mengine katika pambano hilo, yalipachikwa na wachezaji Issa Chole, Sadam Hamisi, Nhingo Juma, Dismas Athanas na Soann Adam.
Katika michuano hiyo Serengeti Boys imepangwa kundi B dhidi ya timu za Uganda, Burundi, Sudan na Djibouti, huku katika kundi A zipo Somalia, Kenya, Sudan Kusini, Rwanda na Ethiopia.




