Na MWANDISHI MAALUMU
WAZIRI Mkuu Dk. Mwigulu Nchemba, amesema ameridishwa na ujenzi wa shule mpya ya bweni, Sekondari ya Sinya.
Shule hiyo iliyojengwa katika Kijiji cha Leremeta, wilayani Longido, Mkoa wa Arusha, imegharimu sh. bilioni 1.23.
Akizungumza na wakazi wa Kata ya Sinya na viongozi mbalimbali waliofika kushuhudia uzinduzi huo, Dk. Mwigulu, alielekeza ujenzi wa uzio wa shule, ufanyiwe kazi haraka kutokana uwepo wa wanyama wakali.
“Nimeridhishwa na ujenzi wa hii shule; taarifa nilizonazo zinaonesha ujenzi wake, umezingatia thamani halisi ya fedha kwa ubora.
“Ombi la kuwekwa uzio hapa shuleni ni jambo la maana kwa sababu, kuna wanyama wakali. “Mkurugenzi angalia ndani ya mapato ya halmashauri, mnaweza kupata kiasi gani ili kazi hiyo ifanywe haraka. Mkuu wa Mkoa (Amos Makalla), simamia jambo hili, liwe moja ya kipaumbele.
“Nyumba za walimu kama alivyoomba mkuu wa shule, Naibu Waziri wa TAMISEMI, kaa nao muangalie uwezekano. Na mabweni yaliyoombwa ni muhimu yajengwe,” alisisitiza Waziri Mkuu.
Awali, akitoa taarifa ya ujenzi, Mkuu wa Shule hiyo, Andrew Emmanuel, alisema shule hiyo ina wanafunzi 387 wa kidato cha kwanza hadi cha tatu na walimu 12, ambao kati yao, tisa wanaume na watatu wanawake.
Alisema bweni la wanafunzi wa kike limekamilika, linatumika na aliomba mabweni zaidi na nyumba za walimu kwa kuwa iliyopo ni moja inayoweza kutumika kwa familia mbili. Alisema nguvu ya wananchi sh. milioni 34, ilitumika kununua meza 140 na vitanda 80.
Katika hatua nyingine, Mwigulu alikagua ujenzi wa mradi wa majisafi wa Sinya–Namanga ambao pia unatekelezwa katika Kijiji cha Sinya, wilayani Longido, mkoani Arusha kwa gharama ya sh. bilioni 13.5.
Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, alisema kupatikana maji katika eneo hilo, kulitokana na uwepo wa mitambo ya kupimia maji chini ya ardhi, iliyonunuliwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambayo iligawanywa katika kanda tofauti.
“Wananchi wa huku walikuwa wanategemea chanzo cha Mto Simba ambacho hakitoshelezi, lakini utafiti uliofanywa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Arusha (AUWSA) ulibaini eneo la Ildonyo (Sinya) linafaa kuwa na kisima chenye uwezo wa kuzalisha lita milioni 2.4 kwa siku,” alisema.
Waziri huyo, alisema uzalishaji wa sasa ni wastani wa lita milioni 1.7 kwa siku, wakati mahitaji ni lita milioni 3.8 na mradi ukikamilika utaongeza uzalishaji hadi lita milioni 4.1 kwa siku, hivyo kuboresha huduma ya maji safi kwa wananchi na mifugo.




