Na AMINA KASHEBA
KOCHA wa Simba, Steve Barker, viwango vinavyoendelea kuonyeshwa na wachezaji wake vinamfanya kutembea kifua mbele na kuwa na uhakika wa kucheza fainali ya Kombe la Shirikisho (FA).
Barker ametoa kauli hiyo saa chache baada ya kuiongoza Simba kuibuka na ushindi wa mabao 4-0, dhidi ya TRA, katika mechi ya robo fainali iliyochezwa Uwanja wa KMC, Dar es Salaam.
Ushindi huo wa kishindo umeipeleka Simba hatua ya nusu fainali ambayo itapambana na Coastal Union, mchezo utaofanyika Juni 20, mwaka huu, katika dimba la Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.
Mabao ya Simba yalifungwa na Clatous Chama dakika ya sita, Anicet Oura dakika ya 26 wakati Selemani Mwalimu alifunga dakika ya 64 na Bashiri Kibaila alimalizia bao la ushindi dakika ya 78.
Akizungumza baada ya mchezo, kocha huyo alisema katika siku za hivi karibuni, wachezaji wake wamekuwa wakionesha viwango vya juu na kupata ushindi ambao unamshangaza.
Alisema pamoja na kukabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa timu pinzani, Simba bado ipo imara na inajua jinsi ya kubadili michezo yake na kupata matokeo mazuri
“TRA United sio timu ndogo, ina kikosi bora lakini ubora wa wachezaji wangu umeizidi timu hiyo ambayo imekuwa ikitoa upinzani mkali Ligi Kuu na FA,” alisema.
Aliongeza kuwa, baada ya kufuzu nusu fainali, anakiandaa kikosi chake kufanya vyema katika hatua hiyo na kukata tiketi ya kucheza fainali.
“Nimefurahi kuona kila mchezaji anafanya kazi yake na kuonesha kiwango kizuri, David Kameta ‘Duchu’ amekuwa mchezaji bora katika mchezo, pia nimefurahishwa na kiwango cha Bashiri Kibaila ambaye amefunga bao la nne,” alisisitiza.
Meneja Habari na Mawasiliano Simba, Ahmed Ally, alisema benchi la ufundi linakwenda kujipanga kujipanga upya kuelekea hatua ya nusu fainali.
“Tunaenda kujipanga kuikabili Coastal Union , tunajua timu hiyo ina wachezaji wenye uzoefu mkubwa, tupo tayari kufika fainali,” alitamba Ally.
Kocha wa TRA United, Etienne Ndayiragije, aliipongeza Simba kwa kucheza vizuri na kupata ushindi.
“Nashukuru Mungu hakuna majeruhi hivi sasa, tunajiandaa na mechi za Ligi Kuu baada ya kutolewa FA,” alisema Etienne.




