Na REHEMA MAIGALA
HOSPITALI ya Taifa Muhimbili (MNH), imeendelea kupiga hatua kubwa ya mafanikio katika utoaji huduma za matibabu, baada ya kuanza kutengeneza matiti ya wanawake wanaokatwa kutokana na kuathiriwa na saratani au ajali.
Huduma hiyo ilianza kutolewa Juni, mwaka huu, ambayo inalenga kurejesha mwonekano wa kawaida wa mwili, kuongeza hali ya kujiamini na kuboresha ubora wa maisha ya wanawake waliopitia matibabu ya saratani ya matiti.
Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Mkuu wa Kitengo cha Upasuaji Rekebishi wa hospitali hiyo, Dk. Laulian Wanyuma, alipozungumza na UHURU.
Alisema katika awamu ya kwanza wamepanga kuwafanyia upasuaji wagonjwa wanne, baada ya miaka miwili iliyopita kuwafanyia operesheni wagonjwa wawili kwa ushirikiano na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha California, San Francisco (UCSF) cha nchini Marekani.
Alifafanua hivi sasa upasuaji huo unafanyika kwa kutumia tishu za mwili wa mgonjwa husika kurejesha umbo la titi lililoondolewa kufuatia kuugua saratani au kupata ajali.
Dk. Wanyuma alisema uamuzi wa kuanzisha huduma hiyo umetokana na ongezeko kubwa la wanawake wanaokatwa matiti kutokana na ugonjwa wa saratani.
“Ongezeko la wagonjwa ni kubwa, ndiyo maana tumeanzisha huduma hii kwa lengo la kuwarejeshea wanawake uasilia wao. Tunataka huduma hii iendelee kutolewa hospitalini hapa (Muhimbili) kwa muda wote,”alisema.
DK. FRANK MUHAMBA
Kwa upande wake, Daktari Bingwa wa Upasuaji Rekebishi wa MNH, Frank Muhamba, alisema pia wanatoa huduma ya upasuaji rekebishi kwa watu wenye matiti makubwa kupita kiasi.
Dk. Muhamba alisema matiti yakizidi ukubwa husababisha maumivu makali ya mabega, shingo na sehemu nyingine za mwili, hali inayowaathiri wanawake kimwili, kisaikolojia na hata kijamii.
Alisema kwa kawaida titi linapaswa kuwa na uzito wa gramu 500, ambapo uzito ukipitiliza kiwango hicho husababisha changamoto za kiafya kwa wahusika.
“Mbali na matatizo ya afya, wanawake wengi hulalamikia kushindwa kuvaa mavazi wanayoyapenda kutokana na ukubwa wa matiti yao, jambo linalopunguza hali ya kujiamini,” alisema.
Dk. Muhamba alieleza wagonjwa wanaofika kupata huduma hiyo ni ambao ukubwa wa matiti yao unasababisha maumivu pamoja na waliopata matiti makubwa kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo kunyonyesha.
MATITI YA KILO NANE
Daktari huyo alisema wanawake wanaopatwa na tatizo la kuongezeka uzito wa matiti ni wenye umri kati ya miaka 25 na 40.
Alisema baadhi yao hufika hospitali wakiwa na titi lenye uzito wa kilo tatu hadi nne, hivyo yote mawili yanaweza kufikia kilo sita hadi nane.
“Matiti ya namna hiyo mara nyingi hufika hadi kitovuni na kusababisha maumivu mabegani na shingoni, kiasi baadhi ya wanawake hushindwa kufanya shughuli zao za kujipatia kipato,” alisema Dk. Muhamba
IDADI YA WANAOHUDUMIWA
Dk. Muhamba alisema Hospitali ya Taifa Muhimbili hupokea wastani wa wagonjwa watatu hadi wanne kila mwezi kwa upasuaji wa kupunguza matiti.
Alisema wanawake wengi wanaopata huduma hiyo ni ambao hawajaolewa.
Kwa mujibu wa Dk. Muhamba, upasuaji huo huchukua kati ya saa tatu hadi nne, baada ya hapo mgonjwa anakuwa salama na kuendelea na hatua za kawaida za kupona.
WATOTO WA KIUME HUATHIRIKA
Dk. Muhamba alisema changamoto kama hiyo pia huwakumba watoto wa kiume, hasa wanapofikia umri wa balehe kutokana na mabadiliko ya homoni.
Alisema baadhi huzaliwa na tatizo hilo, wengine wakipata kutokana na matumizi ya dawa zinazochochea uzalishaji wa homoni zinazopunguza homoni za kiume.
“Tunapata kesi nyingi za watoto wa kiume kujaa matiti ambayo husababishwa sababu nyingi ikiwemo kuzaliwa hivyo au kutumia dawa ambazo zinazalisha homoni zinazosababisha homoni za kiume kupungua.
“Mara nyingi tunawapata vijana hao wakati wa likizo wakifika hapa tunawafanyia operesheni na matiti yao yanarejea kama kawaida,” aliongeza Dk. Muhamba.



