Na Baltazar Mashaka, Mwanza
MGOGORO wa mazishi ya marehemu Wambura Mambya (54), aliyefariki Julai 21, 2026 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza, Sekou Toure, umefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana, huku pande zinazohusika zikionyesha dalili za kufikia maridhiano yatakayowezesha mazishi kufanyika kwa amani.
Shauri hilo la madai namba 19355 la mwaka 2026 lilisikilizwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Wilaya ya Nyamagana, Chrescencia Mushi, likimhusisha mwombaji Elizabeth Nyakao dhidi ya mjibu maombi John Mambya.
Kesi hiyo iliahirishwa hadi Julai 30, 2026 baada ya upande wa ndugu wa marehemu kutokuwapo mahakamani wakati shauri lilipoitwa, huku wakieleza baadaye kuwa walikumbwa na changamoto ya kutofahamu utaratibu wa mahakama.
Baada ya kuahirishwa kwa shauri hilo, mawakili wa pande zote walihitimisha majadiliano yaliyozaa makubaliano ya awali, ambapo ndugu wa marehemu walieleza utayari wao wa kushirikiana ili mgogoro huo umalizike kwa maelewano.
Kwa mujibu wa makubaliano hayo ya awali, mwili wa marehemu unatarajiwa kuzikwa upande wa familia kwa kuzingatia mila na desturi, huku makubaliano hayo yakitarajiwa kuwasilishwa rasmi mahakamani kwa hatua za kisheria.
Akizungumza baada ya mazungumzo hayo, Elizabeth Nyakao alisema ameridhishwa na hatua iliyofikiwa; “nimesamehe na nimeridhika na makubaliano tuliyoyafanya.”
Wakili Demetrius Mtete alisema migogoro ya aina hiyo mara nyingi hupata suluhu kupitia maridhiano ili kulinda maslahi ya pande zote na kudumisha amani katika familia.
Awali, mgogoro huo ulizuka Julai 24, 2026 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekou Toure baada ya ndugu wa marehemu na familia yake kutofautiana kuhusu mahali na utaratibu wa mazishi.
Upande wa mke mkubwa ulieleza kuwa ulitaka kushiriki kikamilifu katika mazishi ya marehemu, huku ndugu wa marehemu wakieleza kuwa walikuwa wakitekeleza maelekezo ambayo walidai marehemu aliwahi kuyatoa kuhusu mahali alipotaka kuzikwa.
Kutokana na hali hiyo, wananchi walikusanyika hospitalini na kusababisha sintofahamu iliyohitaji mamlaka za usalama kuingilia kati ili kurejesha utulivu.
Akizungumza kuhusu tukio hilo, msemaji wa familia Gradson Mambya alisema lengo lao ni kuhakikisha mazishi yanafanyika kwa utaratibu utakaoondoa migogoro na kuimarisha mshikamano wa familia.
Kwa upande wake, Kamanda Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna (DCP) Wilbrod Mutafunga alisema lilichukua hatua za kudhibiti hali ya usalama katika eneo la hospitali baada ya kujitokeza kwa msongamano wa watu na mvutano kati ya pande zinazohusika.
Aidha, kamanda huyo wa polisi wamewakumbusha wananchi kuwa suala la nani mwenye haki ya kufanya mazishi ya marehemu ni miongoni mwa masuala yanayopaswa kuamuliwa na mahakama kwa mujibu wa sheria pale.
Aliwaatakaa wananchi kuepuka kutoa hukumu au kuchukua hatua zinazoweza kuvuruga mwenendo wa shauri, huku akisisitiza kuwa jukumu lao ni kulinda usalama wa watu na mali pamoja na kuhakikisha amani inadumishwa wakati taratibu za kisheria zikiendelea.
Hadi saa 10 jioni, Julai 28, 2026, juhudi za kuwapatanisha pande hizo zilikuwa zinaendelea huku mamlaka zikisisitiza umuhimu wa maelewano kuhakikisha mwili wa marehemu unazikwa kwa amani na heshima.
Mahakama inatarajiwa kuendelea kusikiliza shauri hilo Julai 30, 2026 kwa ajili ya kupokea na kuidhinisha makubaliano yaliyofikiwa na pande mbili zinazohusika, endapo yatakidhi matakwa ya sheria.



