Na ESTA MALIBICHE, Iringa
WAZIRI Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema Serikali itaendelea kumuenzi aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Bunge, Sera, Uratibu na Watu Wenye Ulemavu, marehemu William Lukuvi, kwa kutekeleza yaliyokuwa ndoto yake kwa wananchi wa Jimbo la Isimani mkoani Iringa.
Dk. Mwigulu alisema hayo, alipomwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika maziko ya Lukuvi, yaliyofanyika Kijiji cha Idodi mkoani Iringa.
Alisema Lukuvi atakumbukwa kwa mengi, ukiwemo utumishi wake uliotukuka kwa serikali na utekelezaji wa miradi ya maendeleo jimboni kwake.
Waziri Mkuu Mwigulu alisema Lukuvi alikuwa na ndoto ya kutekeleza miradi mingi kwa wananchi wa Jimbo la Isimani, hivyo serikali itaendeleza ndoto hiyo kuenzi mchango wake.
“Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amenituma kuwahakikishia yote ambayo yalikuwa ni ndoto yake na tamanio lake, yataendelea kutekelezwa ikiwemo ujenzi wa barabara hii ambayo tangu nikiwa Waziri wa Fedha alikuwa akiiombea fedha za ujenzi,”alisema Dk. Mwigulu.
Aidha, Dk. Mwigulu alisema Lukuvi alikuwa kiongozi mwadilifu, mchapakazi kwa serikali, wananchi wake wa Jimbo la Isimani na mzalendo wa taifa, hatua ambayo ilimpa nafasi ya kushika nyadhifa mbalimbali serikalini.
“Tumesikia katika salamu, Lukuvi alikuwa na nidhamu ya juu na utumishi uliotukuka kwa kila nafasi ambayo alipewa, hii inatokana na juhudi zake binafsi za kujituma na kujitolea,”alisema Dk. Mwigulu.
WITO KWA WANANCHI
Waziri Mkuu Mwigulu alitoa wito kwa wananchi wa Jimbo la Isimani kutoingia katika mtego wa kugawanyika kutokana na jimbo hilo kuwa wazi baada ya kifo cha Lukuvi.
“Tunatakiwa kumuenzi Lukuvi kwa kuimarisha umoja, mshikamano kwa watu wa Isimani, tusifanye fujo jimboni,” alisema Dk. Mwigulu.
PADRI MSOMBE
Kwa upande wake, Naibu Baba Askofu wa Jimbo Katoliki la Iringa na Paroko wa Parokia ya Ipogolo, Padri Paulo Msombe, alitoa wito kwa familia, marafiki na wafanyakazi aliofanya nao kazi, kumwombea marehemu Lukuvi kwa kuwa hana uwezo wa kujiombea.
“Tunaambiwa hata katika utoto wake alikuwa mtumishi wa altare, hivyo alikuwa karibu na parokia yake,”alisema Padri Msombe.
SPIKA ZUNGU
Naye, Spika wa Bunge, Mussa Zungu, alisema wabunge zaidi ya 160 walihudhuria maziko ya Lukuvi, ikiwa ni ishara ya mapenzi ya wabunge kwake.
“Nilipata bahati ya kufanya naye kazi, nilivyokuwa Mwenyekiti wa Bunge na baadaye Spika wa Bunge, najua uwezo wa Lukuvi, najua pigo kubwa ambalo bunge limepata kutokana na uwezo, umahiri na utiifu wake kwa serikali.
“Kikubwa ni kumwombea kwa Mungu amsamehe makosa yake na amweke katika makazi mema hadi hapo tutakapokutana naye,” alisema Zungu.
MZEE WASIRA
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Stephen Wasira, alisema Lukuvi hakupenda kuanzia juu, bali alianzia chini katika nafasi za uongozi.
Alisema Lukuvi aliingia chama cha TANU mwaka 1974, miaka mitatu kabla ya kuanzishwa CCM.
Alisema baadaye alijiendeleza katika uongozi wa ngazi ya chini kwa kushirikiana na vijana wenzake na walimwamini hadi kufikia ngazi ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM).
“Mengine yote yalikuja baadaye kwa nafasi ya ubunge, uwaziri, lakini si wengi wanakuwa wabunge na wanalea jimbo na anakuwa waziri na bado analea jimbo,”alisema.
Wasira alisema Lukuvi amekuwa mbunge wa Isimani miaka 31, waziri kwa awamu nne, hivyo kuna jambo la kujifunza kupitia yeye.
“Marais hawa wana watu wengi wa kuwaweka kwenye kazi hizo, hivyo lazima Lukuvi alikuwa ana kitu fulani cha kipekee ambacho marais walikikubali.
Pia, hakusahau utendaji wake CCM, nimefahamiana naye na nimefanya naye kazi mwaka 2005, nilikuwa naye serikalini, tulikuwa kwenye Kamati Kuu hadi mwaka 2017,” alisema.
Wasira aliongeza: “Chama chetu kimepoteza mwanachama mahsusi kwelikweli, ndiyo maana sisi CCM tupo wengi hapa kwa sababu tunatambua mchango wake na mapenzi yake katika Chama chetu.
MAKINDA
Spika mstaafu wa Bunge, Anne Makinda alisema Lukuvi hakuwa mtu wa maneno na hata wabunge wanatambua alikuwa mtu wa vitendo.
“Tukiwa Jumuiya ya Umoja wa Vijana (UVCCM) tulikuwa timu ya mwisho ikimuhusisha Abdulrahman Kinana, Jakaya Kikwete, mimi na wenzetu waliotangulia mbele za haki, tulipoondoka ndiyo walipoingia kikosi hiki cha kina Lukuvi,” alisema Makinda.
Alisema Lukuvi aliwafundisha watu wa Isimani namna ya kufanya kazi, hivyo aliwasihi wasiache kufanya kazi.
“Kufanya kazi bila ya kutegea, bila kinyongo kwa hiyo tujitegemee tusimamie msimamo wa kufanya kazi tujenge nchi yetu, mwenzetu amefanya kwa kipande chake ametangulia,” alieleza Makinda.
MZEE PINDA
Vilevile, Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda, alisema alimtambua Lukuvi yeye akiwa naibu waziri, waziri na waziri mkuu, ambapo alikuwa mtu wa karibu hadi alipostaafu mwaka 2015.
“Hata nilipokuwa kiongozi wa Chama Cha Mapinduzi ambaye ni mlezi wa mkoa wa Iringa kichama, napo nilizidi kushirikiana naye, kitu ambacho nilikuwa nakipenda kutoka kwake ni namna alivyokuwa anajua nafasi yake ya ubunge na uhusiano wake na wapigakura,” alisema.
Alibainisha Lukuvi alijaliwa uwezo mkubwa wa kujenga uhusiano na jamii na alitumia vyema lugha ya Kihehe, hivyo aliwasihi wananchi wa Isimani wajifunze kutoka kwa kiongozi huyo.





