Iramba
NA MWANDISHI WETU
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Stephen Wasira, amekemea viongozi wasiokuwa na msimamo ndani ya Chama, akisisitiza umuhimu wa kuzingatia haki kwa kutoegemea maslahi binafsi.
Amesema CCM inahitaji viongozi wasioyumba katika masuala ya msingi, hivyo wanachama wanapaswa kuwapa uongozi watu wenye sifa za uadilifu.
Wasira aliyasema hayo alipozungumza na viongozi pamoja na wanachama wa CCM wilayani Iramba, Singida, ambapo aliwataka wanachama kuachana na kile alichokiita ‘uchepuko’ na kusimama katika ‘njia kuu’ inayozingatia haki katika uchaguzi wa viongozi ndani ya CCM.
“CCM inahitaji viongozi wenye msimamo katika mambo ya msingi na wasiobadilika kutokana na mazingira au maslahi binafsi. Tunataka uongozi ambao hauyumbi. Tunataka mtu ambaye ana msimamo kwa mambo ya msingi. Huyo ndiye kiongozi wetu,” alisisitiza.
Aliwataka wanachama wa CCM kuhakikisha wanachagua viongozi kwa kuzingatia uwezo, uadilifu na misingi ya haki huku akionya dhidi ya viongozi wanaopatikana kwa rushwa.
Wasira alisema CCM haipaswi kuruhusu uongozi unaotokana na rushwa, vitisho au ujanja wa aina yoyote kwa kuwa viongozi wanaochaguliwa ndiyo wanaokuwa kielelezo cha Chama katika jamii.
“Wanachama ndiyo wenye jukumu la kuhakikisha watu wanaopewa dhamana ya kuongoza Chama wana sifa na uwezo unaohitajika. Sisi ndiyo tunateua wanachama. Msije mkakubali Chama chetu kikapata uongozi unaotokana na rushwa bila uwezo wa kuongoza,” alisema.
Alisema viongozi wa CCM katika ngazi wana majukumu ya kuwateua au kusimamia mchakato wa kupata viongozi wa chini yao, hivyo wanapaswa kuwa waangalifu katika maamuzi wanayofanya.
Wasira alisema wenyeviti wa wilaya wanahusika na uteuzi wa viongozi wa matawi, huku wenyeviti wa mikoa wakiwa na jukumu katika uteuzi wa viongozi ngazi ya kata.
Alionya kiongozi atakayebainika kutumia nafasi yake vibaya kwa kupokea rushwa na kuteua viongozi wasio na uwezo, hatakiwi kuachwa bila kuwajibishwa.
Wasira ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Ndogo ya Maadili ya CCM, alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia utaratibu na misingi ya Chama.
Alisema uwajibikaji unatakiwa kuanzia ngazi za chini hadi Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, kuhakikisha viongozi wanatimiza wajibu wao ipasavyo.
Alisema kiongozi hawezi kutumia utajiri wake kama kipimo cha uwezo wa kuongoza, akisisitiza kuwa fedha haziwezi kuongeza uwezo wa mtu katika uongozi.
UMUHIMU WA KUJITATHMINI
Katika hatua nyingine, Wasira alisema kila kiongozi anapaswa kujipima na kutathmini kama bado ana uwezo wa kuongoza kulingana na mahitaji ya wakati husika.
Alisema uwezo wa kuongoza siyo jambo la kudumu kwa mtu katika maisha yake yote, hivyo kiongozi anapaswa kuwa tayari kumpisha mwingine pale anapoona hana tena uwezo unaolingana na mahitaji ya wakati.
“Huwezi ukasema uwezo wangu umeshuka lakini hela yangu imeongezeka, kwa hiyo hela itaongeza uwezo?. Hakuna. Hela haiongezi uwezo wa kuongoza,” alisisitiza.
Pia, alisisitiza umuhimu wa kuwa na viongozi wenye uwezo wa kukemea na kujibu upinzani kwa hoja, badala ya kutumia vitisho au mbinu zisizo za haki.
Alisema viongozi wa CCM wanapaswa kuchaguliwa kwa hiyari ya wapiga kura, bila rushwa, vitisho wala ujanja wa aina yoyote.
Kwa mujibu wa Wasira, kiongozi anayechaguliwa kwa misingi hiyo anakuwa kielelezo cha Chama kwa wananchi kwa kuwa jamii humtazama kiongozi huyo kama sura ya CCM.
Alisema endapo kiongozi atakuwa mwadilifu, mwenye uwezo na anayezingatia misingi ya Chama, wananchi wataona taswira nzuri ya CCM.




