Na Waandishi Wetu
HATIMAYE ile siku iliyosubiriwa kwa hamu na Watanzania, ni leo, ambayo Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amezindua Bwawa la kihistoria la kuzalisha umeme la Julius Nyerere (JNHHP).
JNHPP ni maono ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, aliyoyajenga na waasisi wenzake kuanzia mwaka 1976, hatimaye leo yametimia chini ya uongozi imara wa Rais Dk. Samia.
Kufuatia tukio hilo kubwa la kihistoria, baadhi ya wanasiasa wakongwe na wachumi; wametoa maoni tofauti kuhusu kukamilika JNHPP, huku wakiwataka Watanzania kutumia fursa ya umeme huo kujiimarisha kiuchumi.
ANNA ABDALLAH
Akizungumza na UHURU, mwanasiasa mkongwe aliyewahi kuwa waziri katika awamu tofauti nchini, Anna Abdallah, alisema, Rais Dk. Samia ameithibitishia dunia uhodari na uchapakazi wake kupitia utekelezaji wa mradi huo, ambao ameundeleza baada ya mtangulizi wake, Hayati Dk. John Magufuli.
“Namshukuru na kumpongeza Rais Dk. Samia kwa uamuzi aliyoufanya wa kuendeleza mradi huu, sasa tunatembea kifua mbele, sio hapa nchini hata Afrika Mashariki na dunia kwa ujumla.
“Ndoto za Mwalimu Nyerere tumeziona zikitekelezwa kupitia Rais Dk. Samia, tumshukuru Mungu kwa kutupa Rais huyu,”alisema.
Alisema mradi huo uliwahi kupangwa kutekelezwa tangu enzi za mkoloni, lakini ulishindikana na ukawa na upinzani.
Kwa mujibu wa Anna, baadhi ya vikwazo vilidai mradi huo utaharibu mazingira, jambo ambalo sio sahihi, kwa sababu sasa maji yameongezeka na uhifadhi umekuwa mzuri.
“Leo historia inaandikwa, hii inatoa ujumbe kwa Waafrika wenzetu kwamba, kuamua kwa usahihi ni jambo muhimu sana, na si kila tunachoshauriwa ni kweli, walituambia mazingira yataharibika si kweli,” alisema.
KATE KAMBA
Mwanasiasa mwingine mkongwe, aliyewahi kuwa Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Kate Kamba, alisema sasa ni wakati wa wananchi kutumia umeme kufanyia kazi fursa mbalimbali zinazotumia nishati hiyo.
“Tusiuangalie umeme, tuangalie fursa zinazotokana na umeme, tujitahidi kufanya mambo ya viwanda, na kuhamasisha kila nyumba iwe na umeme,”alisema.
Pia, alisema Rais Dk. Samia amefanya kazi kubwa ya kukamilisha mradi huo, ikiwemo kutoa fedha na kuhakikisha unakamilishwa.
MZEE JOSEPH BUTIKU
Mwanasiasa mkongwe na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF), Joseph Butiku, alisema kufanikisha kwa mradi huo kumedhihirisha utendaji kazi bora wa Rais Dk. Samia.
Kwa mujibu wa Butiku, hajaona Rais Dk. Samia akishindwa kazi, katika kukamilisha miradi ya maendeleo iliyoko mbele yake.
Alisema Rais Dk. Samia ametekeleza ahadi yake ya kuimalizia miradi mikubwa ya maendeleo iliyoachwa na mtangulizi wake, Hayati Dk. Magufuli.
“Rais wetu anafanya kazi vizuri, nampenda kwa kazi zake na ninatetea kazi nzuri anazofanya, alisema atatekeleza shughuli zote zilizoachwa na Rais Hayati Dk. Magufuli na sasa anatekeleza.
“Na ikumbukwe alifanya kazi na Dk. Magufuli na yeye anaendelea kukamilisha kazi, sisi tushukuru tumepata bwawa na faida zake zinafahamika, sina haja ya kuanza kuzieleza,”alisema.
COASTER KIBONDE
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa chama cha siasa cha upinzani cha Makini, Coaster Kibonde, alipongeza uthubutu wa serikali kwa kujenga bwawa hilo kwa kutumia fedha za ndani.
Mwenyekiti huyo alisema, haikuwa kazi rahisi kwa kuwa baadhi ya mataifa na wakosoaji wa ndani na nje ya nchi walipinga kuwepo kwa mradi huo.
Kibonde alishauri serikali kulinda miundombinu ya bwawa hilo, kuepusha na vitendo vya hujuma kwa kuwa kuna vibaraka wanaoweza kutumwa kufanya hujuma mradi huo.
WAMACHINGA
Mwenyekiti wa Chama cha Machinga Mkoa wa Dar es Salaam, Yusuph Namoto, alisema bwawa hilo litaleta ahueni kwa wajasiriamali, ambao bidhaa zao nyingi wanazouza zinazalishwa viwandani kwa kutumia umeme.
“Tunasema ni faida kwetu hasa wajasiriamali, kwa kuwa bidhaa zetu zinazalishwa viwandani na tutazipata kwa bei nafuu, hii inatokana na viwanda vilivyopo vitatumia umeme kwa gharama nafuu, tofauti na hivi sasa vinatumia gharama kubwa kuzalisha kutokana umeme mdogo,”alisema.
Mwenyekiti huyo, alisema wajasiriamali wadogo wakiwemo wachomeleaji vyuma, saluni za kike, kiume na wauza maji watakuwa na uhakika na ajira zao kwa kuwa umeme utakuwa ukipatikana kwa uhakika.
WACHUMI
Mtaalamu wa Uchumi, Profesa Samwel Wangwe, alisema upatikanaji wa umeme wa uhakika una nafasi kubwa katika kukuza shughuli za kiuchumi, kwa kuwa sekta mbalimbali ikiwemo viwanda, biashara, kilimo na huduma nyingine zinahitaji nishati hiyo kwa lengo la kufanya kazi kwa uhakika.
Profesa Wangwe alisema mradi unaozinduliwa leo, unatakiwa kusambazwa sehemu kubwa nchini kwa lengo la kuleta matokeo mazuri kwa wananachi.
Akizungumzia suala la uwekezaji nchini katika sekta ya umeme, Profesa Wangwe alisema ongezeko la uzalishaji wa umeme linaweza kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini.
“Kila mwekezaji anahitaji umeme wenye uhakika kwa ajili ya kuzalishia bidhaa zake, hivyo mradi huo wa umeme ni moja ya chanzo cha mapato nchini,”alisema.
Aidha, Profesa Wangwe alisema kuwepo kwa mradi huo wa umeme kutaongeza fursa za ajira na kipato kwa wananchi na taifa kwa ujumla.
Pia, Profesa Wangwe alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha umeme unatumika kuongeza thamani ya bidhaa, kukuza viwanda na kuimarisha huduma kwa jamii.
Wangwe alisema mabadiliko ya tabianchi yasirudishe nyuma jitihada za kuzalisha bidhaa kwa kutumia nishati ya umeme.
Aliiomba serikali itumie ubunifu mwingine wa kulinda chanzo cha umeme, ikiwemo kutumia umeme wa upepo na gesi ili shughuli za uzalishaji mali ziweze kuendelea.
PROFESA KINYONDO
Kwa upande wake Mhadhiri wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, Profesa wa Uchumi, Abel Kinyondo, alisema nishati ya umeme ni nguzo muhimu ya uchumi wa taifa.
Profesa Kinyondi alisema nchi yoyote iliyoendelea ni lazima iwe na umeme wa uhakika, ambao utasaidia uzalishaji.
“Hakuna chanzo kingine cha maendeleo dhidi ya nishati ya umeme, ambayo inampa mtu fursa nyingi za uzalishaji mali.
“Nakumbuka binadamu wa kwanza alianza kupata maendeleo baada ya kugundua moto wa kufikicha kijiti na moto ukatokea; baada ya hapo hakuweza tena kula nyama mbichi ila alikuwa anaichoma halafu anakula, hapo ndipo utaona faida ya nishati hiyo,”alisema.
Aidha, Profesa Kinyondo alisema, kuwepo kwa umeme wa uhakika pia ni fursa ya vijana wengi kupata ajira katika viwanda vidogo na vikubwa.
DK.MMARI
Kwa upande mchambuzi wa masuala ya uchumi, Dk. Donald Mmari, alisema mradi huo utaleta mafanikio makubwa mijini na vijijini,
“Wananchi wategemee umeme wa uhakika, kwa sababu uzalishaji mali unategemea nishati hiyo kwa lengo la kufanya kazi kwa urahisi,”aliongeza.
Pia, Dk. Mmari alimshukuru Rais Dk. Samia kwa kufanikisha ujenzi wa mradi huo.
“Tufike mahali tuseme ukweli, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anaweza majukumu mengi aliyoachiwa naona anayatekeleza kwa vitendo,”alisema.
Imeandaliwa na Irene Mwasomola, Rehema Maigala na Saimon Nyalobi




