Na NASRA KITANA
WAKATI kikosi cha timu ya Yanga kikijiandaa kuelekea mkoani Kigoma, kocha wa Simba Steve Barker amesema timu yake inahitaji kuwa makini katika mechi zao na kuacha kuwafikiria Yanga.
Timu hizo zipo katika vita kali ya kila mmoja kutaka kuibuka na ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.
Katika msimamo wa Ligi Yanga inaongoza ligi hiyo ikiwa pointi 60 huku timu ya Simba ikishika nafasi ya pili, ikiwa na alama 58 na kusababisha ushindani kuongezeka.
Yanga imebaki na michezo mitano dhidi ya timu za Mashujaa FC, Fountain Gate FC, Azam FC, TRA United na JKT Tanzania.
Simba wao wamebaki na mchezo dhidi ya Pamba Jiji, Mbeya City, Mtibwa Sugar, Singida Black Stars na KMC.
Kuelekea mchezo wa Juni 13, mwaka huu, Yanga itacheza na Mashujaa FC katika Uwanja wa Lake Tanganyika huku mkoani Kigoma.
Timu hizo, zitashuka dimbani huku Mashujaa FC ikiwa na kumbukumbu ya kupokea kichapo cha mabao 6-0 katika mchezo wa mzunguko wa kwanza uliochezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Simba yenyewe inatarajiwa kushuka dimbani Juni 14, mwaka huu kupambana na Pamba Jiji katika mchezo utakaochezwa Uwanja KMC huku timu hizo zikiwa na kumbukumbu ya kufungana bao 1-1 katika mchezo wa mzunguko wa kwanza.
Kuelekea pambano hilo la Juni 13, mwaka huu, Ofisa Habari wa Yanga, Ally Kamwe alisema timu yao imejipanga vizuri kuhakikisha wanapata ushindi huo kwa vile vita ni kubwa ya kusaka ubingwa huo.
“Tunajua utakuwa mchezo mgumu kwani mechi hizi za mwisho wa msimu mara nyingi zinakuwa ngumu na zenye changamoto kubwa,” alisema.
Kamwe alisema wachezaji wote ambao waliokuwa katika kikosi cha timu ya Taifa wamerejea na wanaendelea na programu ya mazoezi.
Kwa upande wa kocha wa Mashujaa FC, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, alisema hana hofu na Yanga kwani timu yao imefanya maandalizi ya kutosha kupata ushindi.
“Tunajua hautakuwa mchezo rahisi lakini hatutakubali kuona tunapoteza katika uwanja wetu wa nyumbani,” alisema Julio.
Kwa upande wa Simba, kocha Steve Barker akizungumzia kuhusu maandalizi ya kikosi chake kabla ya kuivaa Pamba Jiji alisema wachezaji wake wapo fiti.
“Tunaingia katika mechi zetu zilizobaki tukiwa makini zaidi kwani hatupaswi kuwafikiria Yanga, tunapaswa kuwa makini sisi wenyewe, tufanye vizuri,” alisema Barker.
Hata hivyo, kocha huyo alisema bado muda wa kuzungumzia suala la ubingwa kwa sasa kwani mechi zote zilizobakia ni ngumu na zenye changamoto kubwa.
Meneja habari na mawasiliano wa timu hiyo, Ahmed Ally alisema wamebaki na mechi tano muhimu na lengo lao kubwa ni kuhakikisha wanavuna pointi zote 15.
“Niseme tu ukweli tuna mechi ngumu zilizobakia hakuna iliyokuwa nyepesi lakini kwa ubora tuliokuwa nao kwa sasa inawezekana kuvuna alama 15,” alisema Ahmed.



