NA MWANDISHI WETU, Same
WAZIRI wa Ujenzi, Abdallah Ulega, ameagiza wakandarasi nchini kuwalipa watumishi kwa mujibu wa sheria za nchi.
Waziri huyo ametoa maelekezo kayo jana, akikagua maendeleo ya barabara ya Same- Kisiwani- Mkomazi yenye urefu wa kilometa 100.5 ambayo inajengwa na mkandarasi M/S China Communication Construction Companya Ltd.
Katika tukio hilo alipata malalamiko kuwa wafanyakazi katika ujenzi huo wanalipwa fedha kidogo tofauti na kinachokubalika kisheria.
“Hii haikubaliki. Kuna viwango ambavyo tumekubaliana kwa mujibu wa sheria zetu, ni lazima wakandarasi wote wafuate viwango hivyo. Hilo halina mjadala; alisema Ulega.
Ingawa msimamizi wa kampuni hiyo alimuahidi Ulega suala hilo litafanyiwa kazi, lakini alisema atalifikisha suala hilo kwa Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, ili wamiliki wa kampuni hiyo waitwe nchini na kukubali rasmi kufuata sheria za Tanzania katika malipo.
Katika hotuba yake baada ya ukaguzi huo, Ulega pia alieleza kutofurahishwa na kusuasua kwa mradi huo ulioanza kutekelezwa tangu mwezi Januari, mwaka jana.
” Nilimkabidhi mwenyewe mradi huu mkandarasi mwaka jana, nimetembelea na kuuona, ukweli ni kwamba bado mkandarasi kasi yake ni ndogo hairidhishi na haifurahishi”, alisema Ulega.
Aliongeza kuwa serikali inataka kuona kuwa barabara hiyo inakamilika kwa wakati na ubora ili isaidie kurahisisha shughuli za kijamii na kiuchumi.
Aliwahakikishia wananchi wa Same kuwa ujenzi wa barabara hiyo utaenda sambamba na ujenzi wa vituo na uwekaji wa taa za barabarani kuleta mwanga ili kuchochea shughuli za kibiashara katika maeneo yao.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu alisema kiu ya wananchi wa Same ni kuona barabara hiyo inakamilika ili kuweza kurahisisha shughuli za kiuchumi na kuleta maendeleo katika wilaya hiyo na taifa.
Mradi huo umefika asilimia saba na unagharimiwa na serikali.




