Na NASRA KITANA
USHINDI wa mabao 2-0, ilioupata Simba dhidi ya Azam FC, umemfanya Kocha wa Simba, Steve Barker, kusema kikosi chake kitaendelea kufanya vizuri katika mashindano inayoshiriki msimu huu.
Simba juzi, ilipata ushindi wa ugenini, katika mchezo wa sita wa Ligi Kuu Tanzania Bara, uliochezwa Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.
Katika mchezo huo, Simba ilipata mabao yake kupitia Rushine De Reuck na Clatous Chama.
Akizungumza baada ya mchezo, Barker alisema pamoja na timu kukosa muda wa kujiandaa na mchezo dhidi ya Azam, ilicheza kwa kuelewana na kupambana kwa nguvu kusaka ushindi.
Barker alisema timu ilionesha muunganiko mzuri na kuibana Azam ambayo ilijipanga kuutumia uwanja wa nyumbani kupata matokeo mazuri.
“Nimefurahi kuiona Simba ikipambana kupata ushindi, haukuwa mchezo rahisi, lakini wachezaji wangu walipambana kupata ushindi,” alisema.
Kocha huyo alisema anajivunia kuwa na kikosi imara chenye kiwango bora, ambacho kinaendelea kuimarika kila uchao.
Mchezaji Rushine De Reuck, alisema wamejipanga kyendelea kuipambania timu kwa jasho na damu ili kupata ushindi katika kila mchezo.
“Haukuwa mchezo rahisi kwetu, hatukufanya maandalizi ya kutosha, lakini tulipambana kufanya vizuri na kutimiza lengo,” alisema Rushine.
Kocha wa Azam FC, Florent Ibenge, alisema wachezaji wake walikosa umakini hasa kipindi cha pili na kupoteza pambano.
“Tunajipanga kwa mechi inayofuata baada ya kupoteza pointi tatu kwa Simba, nina imani tutapaya matokeo mazuri katika mchezo ujao,’ alisema Ibenge.
Katika msimamo, Simba inaendelea kusalia nafasi ya pili ikiwa na pointi 18 baada ya kushuka dimbani mara sita huku Azam FC ikishika nafasi ya tatu, ikiwa na alama pointi 14 kibindoni, baada ya kushuka dimbani mara saba.




