Na MUSSA YUSUPH
KATIKA kuhakikisha migogoro baina ya wakulima na wafugaji inabaki historia, mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ameahidi serikali kuja na mpango kabambe kutokomeza kabisa migogoro hiyo nchini.
Amesema mara baada ya kuingia madarakani, Serikali ya CCM itapanua eneo la ufugaji kutoka ekari milioni 3.46 hadi kufikia ekari milioni sita hatua ambayo itapanua wigo wa maeneo ya wafugaji.
Akizungumza wilayani Kilosa (Agosti 30 mwaka huu) katika mwendelezo wa kampeni za Urais, Dk. Samia ameahidi kutatua migogoro baina ya wakulima na wafugaji katika Jimbo la Kilosa kupitia mpango maalumu wa ‘Tutunzane’ ambao tayari umeonyesha mafanikio wilayani Mvomero.
“Serikali itapanua eneo la wafugaji kutoka ekari milioni 3.46 za sasa hadi kufikia ekari milioni sita, hatua ambayo inalenga kupunguza migogoro ya ardhi baina ya wakulima na wafugaji.
Dk. Samia amesisitiza: “Nafahamu zipo changamoto ya migogoro baina ya wafugaji na wakulima ambayo tayari imeanza kufanyiwa kazi, lakini ahadi ya Chama Cha Mapinduzi ni kuendeleza programu ya Tutunzane na kuongeza eneo la wafugaji ili kuepusha migogoro hiyo.”
Kuhusu dira ya taifa ya maendeleo 2050, Dk. Samia amesema Tanzania itakuwa nchi yenye neema itakayotekeleza miradi ya maendeleo pasipo kutegemea mikopo mikubwa huku wananchi wakipata huduma bora za afya, elimu, umeme wa uhakika.
Amesema safari hiyo ya mafanikio itafikiwa katika miaka mitano ijayo hivyo aliwaomba Watanzania kukipigia kura CCM kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29 mwaka huu ili kufanikisha neema hiyo.
“Niwaombe tusimame pamoja kuiunga mkono CCM tuendelee na kasi kujenga Tanzania tunayoitaka. Tukifika mwaka 2050 (kwa mujibu wa dira ya maendeleo ya taifa 2050) tuwe tumeifika Tanzania yenye uchumi wa kipato cha kati ngazi ya juu. Hakuna Mtanzania atakayelia kukosa huduma za afya, elimu wala kukosa umeme.
Amesisitiza: “Tutakuwa na Tanzania ambayo uchumi wake utasimama kujitegemea, hatutaishi wala kufanya shughuli za maendeleo kwa mikopo mikubwa. Na hiyo safari tunaanza miaka mitano inayokuja.”
Dk. Samia amesema ili kufikia azma hiyo, ifikapo Oktoba 29 mwaka huu, wananchi wajitokeze kwa wingi katika vituo vya kupiga kura kukichagua Chama Cha Mapinduzi.




