Na MUSSA YUSUPH
MGOMBEA Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ameahidi kujenga vituo vitano vya afya na zahanati 10 vitakavyoongeza wigo wa upatikanaji huduma za afya kwa wananchi wilayani Gairo.
Dk. Samia ametoa ahadi hiyo wilayani hapo (Agosti 30 mwaka huu) kwenye mkutano wake wa kampeni ambapo alisema katika miaka minne na nusu ya uongozi wake, Gairo imepiga hatua kubwa za maendeleo.
“Tutaimarisha huduma za afya kwa kujenga vituo vya afya vitano katika kata tano na zahanati 10. Pia, tutakamilisha ujenzi wa kituo cha mafunzo ya ufundi stadi (VETA) ili vijana wapate ujuzi utakaosaidia kujiari na kuajiriwa.
Ameongeza: “Katika kipindi cha pili cha miaka mitano, tunakwenda kushughulikia barabara ya Lubeho – Kiswiti, Tabu Hoteli – Kitange, Chakwale – Mtumbatu na Chakwale – Lesaka. Pia barabara nyingine ni Gairo – Nongwe ambayo itakamilshwa.”
Amesema barabara hizo zinakwenda kuwekwa lami sambamba na kuongeza vituo vya afya vingine vitano katika kata za Rubeho, Idigo, Chakwale, Madenge na Leshata.
Kwa upande wa sekta ya mifugo, Rais Dk. Samia amesema serikali yake mara baada ya kuingia madarakani itajenga machinjio ya kisasa manne katika maeneo ya wafugaji.




