Na MUSSA YUSUPH,
Songwe
SHAMRASHAMRA za kishindo cha mapokezi ya Mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Samia Suluhu Hassan, zimetikisa mkoani Songwe.
Zaidi ya wananchi 20,000, wameshiriki matembezi na mbio fupi maalumu kumuunga mkono Dk. Samia kwa namna alivyotekeleza miradi ya maendeleo iliyochangia kuufungua mkoa huo.
Katika matembezi na mbio hizo fupi zilizofanyika, miji ya Tunduma na Vwawa, zikihusisha makundi ya vijana, kinamama na wazee maarufu, wakiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Songwe, Radwell Mwampashi, leo, Dk. Samia, anatarajiwa kuwasili mkoani hapa, kisha kufanya mikutano yake ya kampeni katika miji hiyo, maarufu kwa shughuli za kibiashara.
Akizungumza na waandishi wa habari baada ya matembezi hayo, Katibu Mwenezi wa CCM Mkoa wa Songwe, Komredi Yusuph Rajabu, amesema wananchi, wanachama na wakereketwa wa CCM katika miji hiyo, wamepanga kuvunja rekodi ya kuhudhuria kwa wingi kumsikiliza mgombea huyo wa urais kupitia CCM.
“Songwe tumejipanga, hili ndilo lango kuu la biashara katika ukanda wa SADC, hatuna jambo dogo, leo (jana) tumefanya mbio fupi katika mji wa Tunduma ikiwa ni maandalizi ya kumpokea kiongozi wetu.
“Watu zaidi ya 10,000 tumeshiriki. Mchana tumeshiriki matembezi maalumu katika Mji wa Vwawa, ambako watu zaidi ya 12,000 wameshiriki.
“Watu wengi tupo tayari, tutampokea kwa kishindo, kwa sababu ametuletea neema ya maendeleo katika mkoa wetu,” amesisitiza.
UTEKELEZAJI MIRADI
Miaka minne tangu Dk. Samia kuingia madarakani, mkoa huo, umepata mafanikio makubwa katika sekta ya afya kwa kujengwa hospitali ya rufaa ya mkoa.
“Zamani watu walikuwa wakilazimika kwenda Mbeya kupata huduma za rufaa, lakini sasa huduma zote tunazipata hapa.
“Mwaka 2020, tulikuwa na hospitali mbili za wilaya, lakini hivi sasa zipo tano. “Majengo matatu ya huduma za dharura katika hospitali ya rufaa, yameanza kutoa huduma.
“Kwa upande wa zahanati, mwaka 2020 zilikuwa 155, ila katika miaka minne, zimefikia 214 sawa na ongezeko la zahanati 55,” ameeleza.
Yusuph, amesema mwaka 2020, watumishi wa afya katika mkoa huo, walikuwa 570, lakini kwa miaka minne, Dk. Samia ameongeza idadi ya watumishi kufikia 1,350 ikiwa ni ongezeko la watumishi 780.
Kwa upande wa nyumba za watumishi, alibainisha kuwa, mwaka 2020, zilikuwa 922 ambapo sasa zimefikia 322.
“Mimi ni mwalimu kitaaluma, katika elimu, Dk. Samia ameweka rekodi ya kipekee, kwani idadi ya shule za msingi zimefikia 532 kutoka 455, shule za sekondari zimefikia 155 kutoka shule 120. Madarasa yalikuwa 3,600 lakini sasa yamefikia 4, 272,” alisisitiza.
Akizungumzia ahadi 13 ambazo Dk. Samia aliahidi kuzitekeleza ndani ya siku 100 pindi atakapochaguliwa, alisema suala la ajira 500 kwa sekta ya afya na 7,000 kwa walimu wa hisabati na sayansi, zitatanua wigo wa ajira kwa vijana na kuongeza kiwango cha ufaulu wa wanafunzi katika masomo hayo.
Vilevile, amesema ahadi ya kutoa mtaji wa sh. bilioni 200 kwa wafanyabiashara wadogo, imewagusa wajasiriamali wa mkoa huo, kwani wanaamini watakwenda kuongeza wigo wa mitaji yao kibiashara.
Pia, amesema suala la wahitimu wa mafunzo stadi kupata maeneo ya kuendeleza ujuzi wao, itawasaidia vijana kuendeleza ujuzi wao na kujiajiri kupitia taaluma walizozipata. “Mama hana deni, bali sisi anatudai, maandalizi yamefanyika, wananchi wana matumaini makubwa, hivyo tutampigia kura za heshima.
“Mkoa wa Songwe katika uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji, uliofanyika mwaka jana, tulishika nafasi ya nne kitaifa. “Sasa kwa jambo hili la mama, tunakwenda kushika nafasi ya kwanza kwa wingi wa kura za Rais,” amesisitiza.




