Na NJUMAI NGOTA,
Itilima
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimesema Mgombea Urais wa Chama, Dk. Samia Suluhu Hassan, ameimarisha diplomasia ya kiuchumi na uhusiano mzuri na nchi jirani za kikanda na kimataifa katika miaka minne ya uongozi wake.
Alipoapishwa kuwa Rais Machi 19, 2021, Dk. Samia, aliahidi kulinda umoja, amani, utulivu na amehakikisha nchi inaendelea kuwa nchi moja yenye mshikamano.
Aidha, amewapeleka mabalozi katika nchi mbalimbali, wenye weledi na uzoefu mkubwa kuiwakilisha nchi kimataifa.
Mgombea Mwenza wa Urais kupitia CCM, Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi, ameyasema hayo eneo la Nyakabindi, wilayani Itilima, mkoani Simiyu, katika mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na maelfu ya wananchi.
Amesema Dk. Samia, katika kipindi cha uongozi wake wa miaka minne, amefanya maendeleo makubwa, hizo ndiyo sababu zinazomfanya aendelee kuaminiwa kutokana na mageuzi makubwa ya maendeleo, aliyofanya sekta mbalimbali, zikiwemo za uchumi.
Balozi Dk. Nchimbi, ametaja baadhi ya sababu hizo ni kutekeleza ahadi ilizozitoa Chama na kuzitekeleza kwa vitendo na kuimarisha amani na mshikamano wa kitaifa
Mgombea huyo amesema Dk. Samia, amekidhi matarajio ya Watanzania, ndiyo maana wanatembea kifua mbele kujivunia alama kubwa za maendeleo zilizofanyika kipindi kifupi cha uongozi wake.
Pia, Dk. Samia, amesimamia miradi mikubwa ya kimkakati, ikiwemo ya kumalizia ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mwalimu Nyerere kwa asilimia 100. Alilikuta asilimia 30 na kukamilisha ujenzi wa daraja la Kigongo–Busisi, mkoani Mwanza.
Balozi Nchimbi amesema Dk. Samia, ameboresha afya ya mama na mtoto kwa kujengwa na kuimarishwa vituo vya afya, zahanati na madaktari bingwa wanapatikana kila mkoa.
Kwa mujibu wa mgombea mwenza huyo wa CCM, hivi sasa, mgonjwa halazimiki kusafirishwa kwenda Dar es Salaam na huduma za kitaalamu zinapatikana mikoa yote.
Ameeleza baadhi ya mataifa, yameona matokeo ya mageuzi hayo, hivyo ni wajibu wa Watanzania, kuendelea kumwamini na kumchagua aendeleze kasi ya maendeleo.
MAFANIKIO YA ITILIMA
Balozi Dk. Nchimbi, ametaja baadhi ya mafanikio wilayani Itilima ni pamoja na kuongezeka huduma za jamii, zikiwemo seka za afya, elimu, maji na umeme.
Mafanikio mengine ni hospitali ya wilaya, vituo vya afya vinne, ongezeko la zahanati kutoka 34 hadi 43, shule za msingi kutoka 95 hadi 107 na sekondari kutoka 30 hadi 38.
Amesema hivi sasa, ufaulu wa elimu ya msingi umepanda kutoka asilimia 57 hadi 91 na sekondari kufikia asilimia 97.
ILANI MPYA 2025-2030
Balozi Dk. Nchimbi, ametaja baadhi ya vipaumbele vitakavyotekelezwa katika kipindi cha miaka mitano ijayo wilayani humo ni kujengwa vituo vya afya vitatu, shule za msingi 10, sekondari mpya saba na madarasa 102.
Pia, kuimarishwa miradi ya maji, kuanzishwa kilimo cha umwagiliaji na kuboreshwa miundombinu ya barabara na mazingira ya biashara.
UJUMBE WA MPINA
Akiwa Meatu, Dk. Nchimbi, amemtumia ujumbe aliyekuwa Mbunge wa Kisesa, Luhanga Mpina, asipokipigia kura Chama tawala katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu, atakiuka ahadi yake.
Pia, amemshauri arudishe kadi ya ACT-Wazalendo, atakapofanya hivyo, yeye atakamkabidhi kadi ya CCM.
Kabla ya Mpina kuhamia ACT-Wazalendo, aliwahi kuwaambia wananchi wa Kisesa Balozi Dk. Nchimbi ni kaka yake.
MSIGWA ANENA
Msigwa amesema kutokana na ubabaishaji wa vyama vya upinzani, aliamua kujiunga na CCM ambayo utekelezaji wake wa Ilani ni mzuri.
“Ndugu zangu, msione matashititi, bali ni kupoteza muda, chama pekee kinachoshughulika na matatizo ya watu ni Chama Cha Mapinduzi, kinafanyayia kazi barabara zenu, hospitali, ngozi zenu, pamba na zahanati.
“Mpina nilikuwa naye bungeni mwaka 2010, tukaondoka tukamwacha, naamini atasikia wito wa kaka yake, atarudi, watu wa Kisesa unganeni na Chama Cha Mapinduzi.
Msigwa amesema Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amefanya mambo makubwa kwa taifa kwa kuongeza barabara za lami, hospitali, vifaatiba, ajira na madaraja yamejengwa,”amesema.
KAKA WA MPINA ANENA
Juma Mpina ambaye ni kaka wa Luhaga, aliungana na Dk. Nchimbi, kumtaka mbunge huyo wa zamani wa Kisesa, kurejea Chama Cha Mapinduzi.




