Na LILIAN JOEL,
Arusha
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Steven Wasira, amewataka wanachi wilayani Arumeru, kuchagua wagombea wa CCM kwa kuwa, ndicho Chama chenye Ilani inayotekelezeka.
Wasira, amesema hayo jana, wilayani Arumeru, Mkoa wa Arusha, alipozindua kampeni za mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CCM, Dk. Johannes Lukumay na madiwani wa CCM kutoka kata 27 za jimbo hilo.
“Niwaombe wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi, Oktoba 29 mwaka huu, nendeni mkampigie kura za kishindo Dk. Samia Suluhu Hassan, ambaye amekuwa kinara wa kutekeleza miradi ya kimkakati na miradi mbalimbali ya maendeleo katika kila kata.
“Wakati Dk. Samia anapokea nchi hii, Bwawa la Mwalimu Nyerere la kufua umeme, ujenzi wake ulikuwa asilimia 30 pekee, lakini limekamilika kwa asilimia 100 na changamoto ya mgao wa umeme imeisha,” amesema.
Kwa mujibu wa Wasira, Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2025-2030, imejikita katika uchumi jumuishi, ambao utagusa maisha ya mwananchi ukiwemo ujenzi wa viwanda kila mkoa kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, mifugo na madini.
Amesema miradi mikubwa ya kimakakati likiwemo Bwawala la Nyerere ambalo Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. John Magufuli aliliacha likiwa limefia asilimia 30 pekee huku upatikanaji wa umeme ukiwa Megawati 1,600, sasa limekamilika na umeme unazalishwa zaidi ya Megawati 4,000.
“Ujenzi wa Reli ya Kiwango cha Kimataifa (SGR), unaendelea, umefika eneo la Makutopora, hii itasaidia kusafirisha mizigo mbalimbali kutoka bandari ya Dar es Salaam,” ameeleza.
Kuhusu utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025, alisema vijiji vyote vya jimbo hilo, vimepata umeme.
Amesema katika kipindi cha miaka minne, Dk. Samia amejenga shule mpya za sekondari sita katika jimbo hilo, zenye vyumba vya madarasa 126 na shule mpya za msingi nne.
“Katika sekta ya afya serikali ya awamu ya sita katika Jimbo la Arumeru Mashariki imeshajenga hosptali ya wilaya, vituo vya afya vinne na zahanati 14 hatua hiyo imepunguza vifo vya mama na mtoto,” ameeleza.
Amesema mafanikio hayo yanaiwezesha CCM kuendelea kushika dola kutokana na imani kubwa waliyonayo wananchi kwa serikali ya CCM ambayo inaendelea kubadilisha na kuboresha maisha ya wananchi.
“CCM ni Chama kikongwe ambacho kimeendelea kuaminiwa na wananchi kutokana na kazi kubwa na nzuri, ninyi wananchi wa Arumeru Magahribi na Mkoa wa Arusha ni mashahidi jinsi Chama kilivyonikiwa kuisimamia serikali katika utatuzi wa changamoto zenu,” amesisitiza.




