Na MUSSA YUSUPH,
Singida
SERIKALI ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, imepeleka jumla ya sh. trilioni 1.7 za miradi ya maendeleo mkoani Singida tangu mwaka 2021.
Pia, imewezesha wananchi zaidi ya 500,000 kupata msaada wa kisheria kupitia programu ya ‘Mama Samia Legal Aid’ kwa kufuatilia madai yao na kutatua migogoro ya ardhi.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni za Uchaguzi Mkuu uliofanyika, Uwanja wa Bombadia, Singida Mjini, Dk. Samia, alisema uwekezaji unaofanyika nchi nzima ni kujali utu wa mtu.
“CCM inaweka ilani yake, kuweka uwekezaji kwa kutumia fedha nyingi kama zinavyotajwa, kujali na kuinua utu wa mtu. Tunataka kila Mtanzania tujali utu wake.
Alisisitiza: “Tujali afya yake, tujali elimu yake, tujali usalama wake, tujali kila kitu kinachomgusa Mtanzania hata uchumi na ustawi wake.”
Alisema yote yanayofanyika ni katika kujali utu wa Mtanzania, hivyo aliwaomba Watanzania kuipa ridhaa CCM ili kikafanye makubwa zaidi yanayomjali Mtanzania.
Akizungumzia maendeleo katika mkoa huo, alisema serikali imejenga hospitali nne, vituo vya afya 22 na zahanati 63 lengo ni kusogeza huduma kwa wananchi.
“Najua kuna upungufu wa wafanyakazi, lakini nimeahidi tutakapoingia madarakani mkitupa ridhaa siku 100 za kwanza, tunakwenda kuajiri wafanyakazi wengi katika sekta ya afya na elimu.
“Katika suala la maji, tumepandisha asilimia ya upatikanaji maji, bado mradi wa maji miji 28 unatekelezwa Singida Mjini, Manyoni na Kiomboi.
“Mradi mkubwa utakaomaliza kero ya maji ni ule utakaotoa maji Ziwa Victoria kupita Singida kwenda Dodoma ambao tunaoufanyiakazi na dhamira yetu mkitupa ridhaa tuufanyiekazi kweli kweli ili uje kuondosha kero ya maji,”alisema.




