Na EMMANUEL MOHAMED,
ZANZIBAR
BAADHI ya wananchi Mkoa wa Kusini Unguja, wamesema hawana chama kingine cha kukipigia kura zaidi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ifikapo Oktoba 29, mwaka huu.
Ahadi hiyo waliitoa Uwanja wa Azimio Mtende, katika uzinduzi wa kampeni za CCM, uliohudhuriwa na maelfu ya wananchi kutoka vijiji vya Wilaya za Kusini na Kati, ukipambwa na ngoma na nyimbo za hamasa.
Mkazi wa Kizimkazi, Wilaya ya Kusini, Zainab Kombo Salum alisema CCM imeendelea kushikamana na wananchi kupitia miradi ya maendeleo, ikiwemo barabara, maji safi na huduma bora za afya.
“Hatuna haja ya kujaribu chama kingine, kwa sababu CCM tayari imeonesha matunda yake,” alisema.
Kwa upande wake, Mkazi wa Mtende, Wilaya ya Kusini Unguja, Ali Suleiman Ali alisema CCM imekuwa ikitimiza ahadi zake, hivyo wapo tayari kuendeleza mshikamano huo.
“Oktoba 29 kura zetu zote ni kwa CCM, chama cha ukombozi na maendeleo ya kweli,” alisema.
Mkazi wa Jambiani, Khamis Abdulla alisema vijana wanajivunia
mikakati ya CCM ambayo inawagusa katika sekta mbalimbali, zikiwemo ajira, michezo na miradi ya kujiajiri.
Mariam Khatib wa Kitogani, alisema CCM ni chama kinacholeta mshikamo wa kijamii kupitia utekelezaji wa Ilani zake za Uchaguzi Mkuu.




