NA MWANDISHI WETU, Zanzibar
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kudumisha na kulinda tunu ya amani iliyopo nchini.
Pia, Rais Dk. Mwinyi amehimiza kuendelezwa mshikamano, kuimarishwa upendo na kuondoa aina zote za ubaguzi katika jamii.
Rais Dk. Mwinyi ameyasema hayo, baada ya kushiriki ibada ya Sala ya Ijumaa iliyoambatana na dua maalumu ya kuiombea nchi, viongozi wakuu wa kitaifa na waliotangulia mbele ya haki.
Amesema umoja, mshikamano wa wananchi ni nguzo muhimu ya kudumisha utulivu wa taifa na kila mmoja ana wajibu wa kuchangia kwa vitendo kulinda misingi hiyo.
Dua hiyo iliandaliwa na Ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar kwa kushirikiana na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Juma Malik Akil, imefanyika katika Msikiti wa Mzee Ali Hassan Mwinyi uliopo Mangapwani, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi aliwataka waumini kujiepusha kujiingiza katika makundi yenye viashiria vya migawanyiko au chuki, akisisitiza dini inahimiza amani, uvumilivu na kuheshimiana miongoni mwa wananchi.
Ameeleza mafanikio ya kudumisha amani na utulivu nchini, hususan kipindi cha uchaguzi uliopita, ni kielelezo cha nguvu ya umoja na mshikamano uliopo miongoni mwa wananchi, ambapo hali ya utulivu ilidumu katika hatua zote za mchakato wa uchaguzi kutokana na ushirikiano na uelewano huo.
Aidha, amesema ni wajibu wa kila muumini kuwaombea wazee, ndugu na jamaa waliotangulia mbele ya haki, akieleza miongoni mwa mambo yenye manufaa kwa marehemu ni dua za wale waliobaki hai.
Dua hiyo ilihudhuriwa na Mke wa Rais wa Zanzibar, Mariam Mwinyi, viongozi mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, viongozi wa dini, ndugu, jamaa na marafiki.
Katika hatua nyingine, Rais Dk. Mwinyi, akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali wa serikali na waumini, walizuru kaburi la Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi kumwombea dua maalumu.




