Na AMINA KASHEBA
BAADA ya kutinga hatua ya robo fainali ya Kombe la FA, Kocha wa Simba, Steve Barker, amesema amefurahishwa na kiwango kizuri kilichoonyeshwa na wachezaji wake katika mchezo dhidi ya Dodoma Jiji.
Simba ilipata ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Dodoma Jiji juzi katika mchezo wa hatua ya 16 bora ya Kombe la FA katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha.
Akizungumza baada ya mchezo huo, Barker alisema amefurhishwa na kiwango kizuri kilichoonyeshwa na wachezaji wake.
Alisema timu yake ilistahili ushindi huo kwa kuwa ilikuwa katika kiwango chenye ubora wa hali ya juu.
“Nilikuwa nina imani kuwa tutafunga na kushinda mechi kutokana na ubora wa wachezaji wangu, nimefurahishwa sana na matokeo haya ambayo yametupeleka hatua ya robo fainali,” alisema.
Kocha huyo alisema baada ya kumaliza kibarua dhidi ya Dodoma Jiji, hivi sasa anarudi uwanja wa mazoezi kukiandaa kikosi kwa mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Fountain Gate itakayopigwa kesho katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.




