Na SELINA MATHEW, Dodoma
SERIKALI imewahakikishia Watanzania kuwa maandalizi ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwakani, yanaendelea kama yalivyopangwa na hakuna sababu ya kuwa na hofu juu ya kufanyika kwake.
Hayo yalisemwa jijini Dodoma na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, alipozungumza na waandishi wa habari.
Makonda alisema Tanzania ipo katika hatua nzuri ya maandalizi ya michuano hiyo mikubwa kwa soka Afrika.
Makonda alieleza kuwa, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu, huku mkandarasi akiwa tayari kazini kuhakikisha kila kitu kinakamilika kwa wakati.
Alisisitiza kuwa taarifa zinazosambaa mitandaoni kuhusu uwezekano wa kuahirishwa kwa mashindano hayo hazina ukweli wowote na ni sehemu ya upotoshaji.
“Maneno yanayotapakaa mitandaoni, kejeli na mipango miovu ya kutaka kuhalalisha kuahirishwa kwa AFCON kamwe hayatapata nafasi, ratiba iliyopangwa ipo vilevile,” alisema.
Aliongeza kuwa, Rais wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na timu yake walishakubaliana na maandalizi ya Tanzania kuwa mwenyeji na fedha zote muhimu tayari zimeshalipwa kuhakikisha mashindano yanafanyika nchini.
Hata hivyo, alisema mijadala inayoendelea mitandaoni ina mchango chanya kwani inachochea ari na kuwakumbusha Watanzania kuwa muda wa mashindano unakaribia, huku akisisitiza kuwa ratiba ipo palepale.




