Na IRENE MWASOMOLA
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA), imeendelea kuvunja rekodi ya ukusanyaji mapato, baada ya kusanya sh. trilioni 9.8 kuanzia Oktoba hadi Desemba, mwaka jana.
Pia, imeandika historia mpya ya kukusanya sh. trilioni 4.130 mwezi Desemba pekee, ikilinganishwa na sh. trilioni 3.5 zilizokunywa kipindi kama hicho mwaka 2024.
Aizungumza Dar es Salaam, Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, amesema ukusanyaji wa sh. trilioni 9.8 umevuka lengo lililokusudiwa ambalo ni sh. trilioni 9.6.
“Tulipaswa kukusanya shilingi trilioni tisa na bilioni 660, lakini tumekusanya shilingi trilioni tisa na bilioni 800, hiki ni kiasi kikubwa ni ufanisi wa asilimia 101.2 ,”amesema Kamishna Mwenda.
Kamishna Mwenda alisema Desemba mwaka jana, waliweka lengo la kukusanya sh. trilioni 4.14, lakini walivuka lengo na kufikia trilioni 4.130 mafanikio ambayo hayakuwahi kutokea tangu kuanzishwa mamlaka hiyo.
“Kiasi hiki ni kikubwa ni mara ya kwanza hakijawahi kukusanywa na TRA kwa mwezi mmoja, mwaka jana mwezi kama huo (Desemba 2024) tulikusanya shilingi trilioni tatu na bilioni 500,”amesema.
Vilevile Kamishina Mwenda alisema, wastani wa ukusanyaji kodi kwa mwezi umepanda kutoka sh. trilioni 2.7 hadi sh. trilioni 3.130 kwa mwezi.
Kamishina Mwenda alisema mafanikio hayo yametokana na uhimilivu wa uchumi uliopo nchini, sera za uchumi, ulipaji kodi kwa hiyari na mfumo mzuri wa kodi uliowekwa.
Pia, Kamishina huyo alitaja sababu nyingine zilizochangia mafanikio hayo ni jitihada za utendaji kazi mzuri kwa watumishi wa TRA.
“Tunamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kujenga uchumi himilivu, mwezi Oktoba pamoja na changamoto hatukushuka kiwango tulichotakiwa kukusanywa na mwezi Novemba hatukushuka,”ameongeza.
Aidha, Kamishna Mwenda amesema mwaka huu TRA imejipanga kusimamia sheria za kodi, kupambana na wakwepa kodi na kuendelea kusimamia uadilifu kwa watendaji wa mamlaka hiyo.
“Tutaimarisha sana watumishi wetu na kusimamia uadilifu katika utendaji kazi,”ameongeza.
Aidha Kamishina Mwenda amesema TRA imejipanga kuboresha huduma zake,ambapo inatarajia kuanzisha mfumo mpya wa kodi za ndani utakao anza Januari mwaka huu.
“Kupitia mfumo huo mambo mengi yatafanyika ‘online’ ule usumbufu wa walipa kodi kwenda kwenye ofisi zetu utapungua sana.
“Tutakuwa na maamuzi ya kikodi ambayo ni ‘data base’ tofauti na awali,”amesema Kamishna Mwenda.
Amesema mfumo huo utafanywa kidijitali hatua ambayo itarahisisha utendaji kazi, kuboresha huduma kwa walipa kodi na kuondoa malalamiko.
Kamishna Mwenda amesisitiza TRA itaendelea kushirikiana na walipa kodi kwa kuwezeha katika shughuli zao za biashara na kuendelea kuwasikiliza.
Vilevile, Kamishna Mwenda ametoa rai kwa wananchi kuendelea kulipa kodi kwa hiyari kwa mustakbali wa maendeleo ya taifa.




