Na NASRA KITANA
WAKATI kikosi cha ‘Taifa Stars’, kikitarajiwa kushuka dimbani kesho dhidi ya Morocco, Kocha wa timu hiyo, Miguel Gamondi amesema amefanya uboreshaji wa kikosi chake kuhakikisha wanapapata ushindi na kuandika rekodi.
Stars inatarajiwa kushuka dimbani kesho katika mchezo wa hatua ya 16 bora ya mashindano ya Mataifa ya Afrika (AFCON 2025), dhidi ya Morocco mechi itakayofanyika Uwanja wa Prince Moulay Abdellah uliopo Rabat, nchini humo kuanzia saa 1:00 usiku.
Akizungumzia maandalizi ya mchezo huo, Kocha Gamondi alisema wamejipanga vyama kuhakikisha wanafanya vizuri na kujiwekea mazingira mazuri ya kusonga mbele katika michuano hiyo msimu huu.
Alisema katika kikosi chake amefanya maboresho tofauti na kilichocheza mechi ya mwisho ya hatua ya makundi dhidi ya Tunisia ambapo walitoka sare ya mabao 1-1.
Gamondi alisisitiza anatambua ugumu wa mchezo huo kwani wanakwenda kukutana na timu yenye kiwango cha juu, hivyo watapambana kuhakikisha wanapata ushindi na kuendelea kulipaisha soka la Tanzania kimataifa.
Alisisitiza katika mazoezi waliyofanya pia alipata nafasi ya kukaa na wachezaji wake na kuwajenga kisaikolojia kuhakikisha wanacheza kwa utulivu katika mechi hiyo na kwamba wanaamini watafanya vizuri na kufikia malengo waliyojiwekea.
“Kikosi chetu kipo tayari kwa ajili ya kuandika historia nyingine katika soka la Tanzania, tunajua Morocco watakuwa na mashabiki wengi, watatupa presha, lakini sisi tutahakikisha tunapambana ili kufikia malengo.
“Tunachohitaji ni ushindi katika mchezo uliopo mbele yetu ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kusonga mbele zaidi.
“Nimelazimika kufanya uboreshaji wa kikosi kwa kiasi fulani baada ya kubaini makosa madogo madogo katika mchezo wa mwisho hatua ya makundi dhidi ya Tunisia,” alisema Gamondi.
Kocha huyo alisema wachezaji wote wana morari ya kutosha na kila mmoja anajua nini anatakiwa kufanya ili kuisaidia timu kuibuka na ushindi na kusonga mbele.
Naye Ofisa Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Clifford Ndimbo alisema kuwa wachezaji wote wanaendelea na mazoezi kwa kufuata programu za benchi la ufundi.
Alisema wachezaji wawili walipata majeraha ambao ni Yacoub Suleiman na Abraham Morice lakini hali zao zinazidi kuimarika kwani wanapatiwa matibabu na jopo la madaktari.
Alisema kuwa kila mchezaji anajua majukumu yake na wote waemeahidi kupambana na kuhakikisha timu inapata matokeo mazuri na kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania katika fainali za msimu huu.
“Kikosi chetu kinaendelea vizuri na programu za benchi la ufundi, wachezaji wana hali nzuri isipokuwa majeruhi wawili, lakini wengine wameahidi kupambana kuhakikisha timu inapata ushindi,” alisema Ndimbo.
Stars ilianza mechi zake za kundi C kwa kukubali kufungwa mabao 2-1 dhidi ya Nigeria, kabla ya kufungana 1-1 na Uganda huku ikimaliza hatua ya makundi kwa sare ya 1-1 dhidi ya Tunisia.




